Na Sophia Kingimali.
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan ameonesha kwa vitendo kuwa ni mfariji wa taifa kwa kuwanunulia vifaa vya shule wanafunzi wote wa walioathirika na maporomoko ya tope wilayani Hanan’g, mkoani Manyara, Desemba 3, mwaka huu.
Akizungumza jijini Dar es Salaam leo januri 5,2024 Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo,Mobhare Matinyi amesema ikiwa zimebaki siku mbili wanafunzi kufungua shule, serikali imehakikisha watoto wote wa eneo la maafa wanapata sare mpya za shule ikiwa ni mashati, sketi, kaptula, viatu, mabegi, madaftari kwa kufuata viwango vya madarasa waliyopo watoto hao.
Amesema Shule tatu zilizokuwa kambi za waathirika pamoja na shule iliyokuwa ikitumika kama ghala la kupokelea na kuhifadhia misaada sasa zimewekwa tayari kupokea wanafunzi wanaofungua shule.
“Zile Kambi zilishafungwa na uongozi wa wilaya umeandaa ghala lingine kwa ajili ya kuhifadhia misaada inayopokelewa kutoka kwa wadau mbalimbali,” amesema.
Akizungumzia ujenzi wa nyumba za makazi Matinyi amesema serikali imeanza utekelezaji wa ahadi ya Rais, Dk. Samia ya kuwajengea waathirika wa maafa Hanang, mkoani Manyara wa jumla ya nyumba 101 ambapo 89 zilizothibitika kupotea baada ya maafa na 12 ambazo wataalam wa serikali wameshauri zibomolewe na eneo lake lisitumike kwa ajili ya makazi ama shughuli zozote za kiuchumi na kijamii.
“Serikali imetenga ekari 100 kwa ajili ya ujenzi wa makazi mbadala ya kudumu katika shamba la Waret lililopo katika eneo la Jeshi la Magereza, kwenye kijiji cha Gidagamowd, kata ya Mogitu, wilayani Hanang. Eneo hilo lipo umbali wa kilomita 4.5 kutoka barabara kuu ya Babati-Singida, na kilomita 21.2 kutoka mji mdogo wa Katesh kuelekea Singida,” amesema.
Aidha Matinyi amesema kuwa kazi zilizokamilika hadi sasa ni upimaji wa viwanja na usajili wa ramani ya eneo la ujenzi ambapo kuna jumla ya viwanja 269 vilivyopimwa , 226 ni makazi pekee, 26 ni makazi na biashara,17 ni maeneo ya huduma za kijamii.
Amesema hatua inayofuata ni umilikishaji wa viwanja kwa waathirika, ukamilishaji wa ubunifu wa ramani za nyumba, gharama na zijengwe na nani huku mpango ni kufanya kazi kwa mtindo wa operesheni kwa muda wa miezi mitatu.
Sambamba na hayo amesema Zoezi la uhamaji kwa hiari kwa wananchi wanaoishi ndani ya eneo la hifadhi ya Ngorongoro linaendelea vyema ambapo leo Januari 5,2023 kundi la kaya 30 zenye watu 224 na mifugo 393 limehamia kijijini Msomera.
“Hili ni kundi la kwanza katika awamu ya pili la wananchi wanaohamia Msomera. kundi hili linakwenda kuungana na wananchi wengine 3,010 kutoka kaya 551 zenye mifugo 25,521 ambao walihamia awamu ya kwanza baada ya nyumba 503 kukamilika kijijini Msomera,” amesema.
Amesema serikali inaendelea kusisitiza kwamba zoezi hili ni la hiari kwa sababu ni kuwahamishia wananchi wa Ngorongoro katika eneo lililokuwa bora kwa maendeleo yao.
AKIZUNGUMZIA WAKIMBIZI
Serikali imekanusha taarifa zinazoendelea kwenye mitanda ya kijamii za mkimbizi wa Rwanda kutekwa nchini.
Matinyi alisema hadi sasa Tanzania ina jumla ya wakimbizi 200,000 waliokubaliwa huku watu 40,000 wakiomba haki ya ukimbizi nchini .
KUHUSU SGR
Kwa upande mwingine,Matinyi amesema reli ya Kisasa(SGR) inatarajia kuanza kutumika kabla ya Julai, mwaka huu kwa sababu taratibu zilizobaki ni kumalizia vitu vidogo .
Amesema baada ya kukamilika utaanza safari zake katika mikoa ya Morogoro na baadae kwenda hadi Dodoma.
Pia amesema ukamilishaji wa reli ya mizigo utakapokamilika Tanzania itakuwa ndiyo nchi itakayokuwa na reli ndefu kuliko zote barani Afrika.