Mkuu wa Wilaya ya Rungwe Mhe.Jaffar Haniu leo tarehe 5.1.2024 amezindua zahanati ya Ilenge iliyopo katika kata ya Kyimo ikiwa ni mwendelezo wa kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya afya karibu na Makazi yao.
Akizindua Zahanati hii , Mhe Haniu amewashukuru Wananchi kwa ushirikiano waliouonesha katika ukamilishaji jengo hili na kuwa jitihada hizi zinatakiwa kuigwa katika maeneo mengine.
Aidha ameishukuru Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa kiasi cha shilingi million 50 kwa ajili ya ukamilishaji wa jengo la zahanati pamoja na shilingi million 25 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba.
Amesema katika vipindi tofauti serikali imekuwa ikitoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya afya hatua inayotakiwa kila mkazi wa wilaya ya Rungwe kutambua na kushiriki ili kuhakikisha inakamilisha kwa wakati.
Katika hatua nyingine amewapongeza watumishi wa afya kwa kazi nzuri wanayofanya katika kuhudumia jamii huku akionya wale wachache wanaokiuka miiko na maadili ya kazi yao kuwa kufanya hivyo kunawanyima haki wananchi ambao wametoa jasho lao kujenga miundombinu hiyo.
Kwa upande wa miundombinu ya barabara na umeme inayoingia katika zahanati hii, Mhe Haniu ameahidi kuifanyia kazi ili wananchi waendelee kupata huduma nzuri na salama katika mazingira mazuri.
Akizungumzia usajili wa wanafunzi wa darasa la kwanza na Kidato cha Kwanza, Mhe.Haniu ameagiza wazazi wote wenye watoto wenye sifa ya kujiunga na darasa la kwanza pamoja na kidato cha kwanza kuhakikisha wanawapeleka shule ifikapo januari 8 mwaka huu huku walimu wakiwapokea bila masharti yoyote .
“Serikali imejenga vyumba vya madarasa katika maeneo mbalimbali na elimu ni bure kwa kila mwanafunzi.Michango ni michache kadri nyie wazazi mlivyokubaliana katika vikao vyenu halali. Hivyo niagize watoto wote waripoti katika shule zao ifikapo tarehe 8 wiki ijayo.” Ameeleza.
Katika Hatua nyingine Uongozi wa Chama cha Mapinduzi kata ya Kyimo umeipongeza serikali kwa kuiletea kata hii miradi lukuki hali inayozidi kutengeneza mazingira mazuri ya wananchi kupata huduma mbalimbali.
Baadhi ya miradi ni pamoja ujenzi wa kituo cha afya Kyimo, Shule mpya ya Mchepuo wa Kingereza Ilenge, ukamilishaji wa vyumba vya madarasa katika shule ya Msingi syukula, Katabe, Kibisi na Salemu, Ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule ya sekondari Kyimo na Ufunguzi wa shule mpya ya Sekondari Kibisi.
Wakati huohuo Askofu Mstaafu wa kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Konde Mchungaji Dkt Israel Mwakyolile ameipongeza Menejimenti ya Halmashauri ya wilaya ya Rungwe kwa kusimamia miradi ya maendeleo ipasavyo kwani kila kona thamani ya fedha na muonekano wa mradi vinawiana.