Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Kamishina Msaidizi wa Polisi Pius Lutumo, amewataka wakaguzi wa Polisi kuheshimu kiapo walichoapa katika utendaji kazi wao.
Kamanda Lutumo ameyasema hayo,wakati wa kufunga mafunzo ya kuwajengea uwezo wakaguzi wa Polisi kwenye viwanja vya Polisi Mkoa wa Pwani yaliyofanyika kwa muda wa miezi miwili.
Kiapo cha askari ni utii kwa Serikali iliyo madarakani na kuwaheshimu viongozi wote ikiwa ni pamoja na kuheshimu viongozi wa Jeshi katika kada ya vyeo mbalimbali.
Amewaeleza wakaguzi hao wanajukumu la kwenda kusimamia nidhamu na maadili ya askari katika utoaji wa huduma bora kwa wale wanaofika vituo vya Polisi kwenye maeneo yao.
“Tumeapa kuwatumikia wananchi lakini bado wapo baadhi ya askari wamekuwa wanasahau viapo vyao, hivyo muende mkawe wa kwanza kubadilika kifikra ili wale mnao wasimamia nao waweze kufuata nyayo zenu”.Alisema Lutumo
Aidha, Kamanda Lutumo amewakumbusha umuhimu wa kila mkaguzi kwenda kushirikiana na viongozi wa Serikali na wadau wengine kwenye kuzuia na kutanzua uhalifu kwenye Kata zao.
Jukumu la kuwalinda watoto na kupambana na vitendo vya ukatili lipo kwenu, “nendeni mkashirikiane na taasisi zingine kwenye kupata matokeo chanya katika kesi zilizo kwenye himaya zenu za ukatili badala ya kesi hizo kumalizwa kienyeji.
Kadhalika, wakaguzi hao wametakiwa wakafanye kazi zao kwa kuzingatia vithaminiwa vinne vya Jeshi la Polisi kwenye maeneo yao ya kazi yaani Nidhamu,Haki, Weledi na Uadlifu.
Nae mshiriki wa mafunzo hayo ya kuwajengea uwezo wakaguzi,Mkaguzi wa Polisi Rosemary Kamugisha akiongea kwa niaba ya wakaguzi wenzake amesema miezi miwili waliyokuwa kwenye mafunzo wameweza kujifunza mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kesi zitakazo funguliwa mahakani zinapata matokeo chanya.