
Na Victor Masangu, Kibaha
Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dkt. Nicas Mawazo amewahimiza wazazi na walezi kuachana na tabia ya kuwatelekeza watoto wao hasa katika suala zima la kuwaendeleza kielimu na badala yake washiriki kikamilifu katika kuwa mstari wa mbele kuchangia maendeleo katika kuboresha sekta ya elimu na sio kubaki nyuma.
Kauli hiyo imetolewa na mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha wakati wa mahafali ya 16 shule ya msingi Lulanzi Dkt. Nicas Mawazo ambapo amewahimiza wazazi wanapaswa kuweka misingi imara ya kuchangia elimu kwa ajili ya kuweza kuwasaidia watoto wao wasome katika mazingira mazuri na kutimiza ndoto zao ambazo wamejiwekea.
“Kwanza nimefarijika sana kualikwa katika mahafali haya ya darasa la saba katika shule ya msingi Lulanzi lakini kitu kikubwa ambacho ninawaomba wazazi na walezi ni lazima tushirikiane kwa pamoja katika suala zima la kuweza kuchangia mambo mbali ya kielimu na lengo kubwa ni kwa ajili ya watoto wetu ikiwa sambamba na kuboressha miundombinu ya shule pamoja na ujenzi wa ofisi za walimu,”amebainisha Mstahiki Meya.
Mstahiki Meya huyo amebainisha kwamba lengo lake kubwa ni kuendelea kushirikiana bega kwa bega na wazazi pamoja na walezi kwa lengo la kuleta mabadiliko chanya ya kuboresha elimu katika shule mbali mbali zilizopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha na kuahidi kuendelea kutoa sapoti lengo ikiwa ni kuweka mipango madhubuti ya kukuza elimu na wanafunzi kusoma katika mazingira mazuri.
Kwa upande wake Mkuu wa shule ya msingi Lulanzi Bakari amesema kwamba shule hiyo inakabiliwa na changamoto mbali mbali ikiwemo sula la kukosa uzio pamoja na mahitaji mengine ya msingi hivyo ameimba serikali kuweza kuwasaidia kwa hali na mali ili walimu na wanafunzi waweze kusoma katika mazingira ambayo ni rafiki.
Naye mmoja wa wanafunzi ambao wamehitimu katika shule hiyo Janeth Mwangi akisoma risala kwa niaba ya wanafunzi wenzake amebainisha kwamba shule hiyo tangu ianzishwe mnamo mwaka 2007 imeweza kupata mafanikio makubwa ikiwemo katika kufanya vizuri katika nyanja ya kitaaluma pamoja na uboreshaji wa mazingira ya shule.
“Tangu shule hii ilipoanzishwa mnamo mwaka 2007 imeweza kupiga hatua kubwa sana ikiwemo suala la uboreshaji wa miundombinu ya shule japo tunakabiliwa na uhaba wa fedha kwa ajili ya uendeshaji wa shule, uwepo wa wingi wa wanafunzi upungufu mbali mbali wa vifaa vya taaluma,”amebainisha Mwalimu huyo.
Mahafali ya 16 ya shule hiyo ya msingi ya Lulanzi iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha imeweza kuhudhuliwa na wageni mnbali mbali wakiwemo viongozi mbali mbali wa serikali, viongozi wa chama pamoja na wazazi na walezi kwa lengo la kuweza kushiriki na kujumuika katika mahafali hayo ya darasa la saba.
