Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo (Mb), amepokea Nakala za Hati za Utambulisho kutoka kwa Balozi Mteule wa Ubelgiji nchini Mhe. Lot Debruyne, katika Ofisi ndogo za Wizara, Jijini Dar es Salaam.

Baada ya tukio hilo viongozi hao walijadili namna bora ya kuendelea kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na ushirikiano kati ya Tanzania na Ubelgiji.

Akizungumza na Balozi Mteule wa Ubelgiji Mhe. Waziri Kombo alisisitiza azma ya kuhamisha ushirikiano kutoka kwenye misaada na kuelekea katika kufanya biashara na uwekezaji.

Mhe. Waziri Kombo ameeleza juu ya fursa za ushirikiano katika kilimo na umwagiliaji, uhamishaji wa maarifa na ujuzi, pamoja na mitambo na teknolojia za kisasa za kilimo.

Pia alihimiza kuongezwa kwa biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Ubelgiji akitaja ongezeko la watalii kupitia safari za moja kwa moja za Shirika la Ndele la Ubelgiji (Brussels Airlines) kwenda Kilimanjaro na Zanzibar kama fursa ya kukuza sekta ya utalii.

Viongozi hao walibainisha maeneo ya ushirikiano ikiwemo ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi, nishati safi na jadidifu, mapishi safi, mabadiliko ya kidijitali na afya.

Aidha, viongozi hao walisisitiza juu ya ushirikiano kati ya Bandari za Antwerpen na Dar es Salaam, pamoja na fursa za ushirikiano kati ya Chuo Kikuu cha Ghent na taasisi za Tanzania katika kukuza matumizi ya lugha ya Kiswahili.