Mchumi kutoka Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPU), Wizara ya Fedha, Bi. Anastazia Amandi, akitoa ufafanuzi kwa wananchi kuhusu masuala ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), walipotembelea katika Banda la Wizara ya Fedha, wakati wa Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayofanyika katika Viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Mchumi Mkuu, Idara ya Sera, Wizara ya Fedha, Bw. Lelansi Mwakibibi, akitoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu ya Idara hiyo, walipotembelea katika Banda la Wizara ya Fedha wakati wa wakati wa Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayofanyika katika Viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Picha za matukio mbalimbali katika Banda la Wizara ya Fedha, wakati wa Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayofanyika katika Viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dar es Salaam)
…………..
Na. Asia Singano na Saidina Msangi, WF – Dar Es Salaam.
Serikali imesema itatekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kwa utaratibu wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), ikiwemo miundombinu ya usafiri ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma mbalimbali kwa wakati.
Hayo yameelezwa na Mchumi kutoka Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPU), Wizara ya Fedha, Bi. Anastazia Amandi, alipokuwa akieleza wananchi kuhusu majukumu ya Kitengo cha PPP, waliotembelea katika Banda la Wizara ya Fedha, wakati wa Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayofanyika katika Viwanja vya Mwl. J. K Nyerere, jijini Dar es Salaam.
Alisema Serikali imefanya maboresho ya Sera, Sheria na Kanuni za PPP ili kuimarisha mazingira ya uwekezaji na kuongeza ushiriki wa Sekta Binafsi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambapo hadi Juni mwaka 2026, jumla ya mikataba tisa ya PPP imesainiwa kutoka sekta mbalimbali za maendeleo.
‘’Miradi iliyosainiwa ni Manasi yaendayo Haraka Dar Es Salaam (DART), awamu ya kwanza na ya pili yenye mikataba minne, ikiwemo Mradi wa Ukaguzi wa Lazima wa Vyombo vya Moto na Mradi wa Ujenzi na Uendeshaji wa Jengo la Biashara Kariakoo (DDC)’’, alisema Bi. Amandi.
Alisema miradi mingle ni pamoja na Ukarabati na uendeshaji wa Reli Ya Tanzania na Zambia (TAZARA), pamoja na Uboreshaji bandari ya Dar Es Salaam kupitia kampuni za DP World na ADAN.
Aliongeza kuwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa njia ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), una tija kubwa ndio maana Serikali imeona umuhimu wa ushirikiano na sekta binafsi kama ilivyopewa kipaumbele katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
‘’PPP ina faida nyingi sana ikiwemo kupata mtaji kutoka Sekta Binafsi na hivyo kupunguza utegemezi wa Bajeti ya Serikali katika kutekeleza miradi ya maendeleo, kupata ujuzi, utaalamu na teknolojia kutoka Sekta Binafsi, kuwezesha upatikanaji wa ajira na mapato kwa Serikali, kuboresha upatikanaji wa huduma kwa ufanisi na kwa wakati pamoja na mgawanyo wa vihatarishi ambavyo kwa kiasi kikubwa vinabebwa na Sekta Binafsi’’ aliongeza Bi. Amandi.
Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayofanyika katika Viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam, kuanzia Juni 28 hadi Julai 13, ni maonesho ya 50 toka kuanza kwake ambapo yanaambatana na kuadhimisha miaka 50 ya maonesho hayo.
