Mchumi Mwandamizi, Wizara ya Fedha, Bi. Consolata Komba, akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayofanyika katika Viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam, yakiwa na Kaulimbiu kuu “Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania”.

Mhasibu Mkuu Daraja 1, Wizara ya Fedha, Bw. Peter Rushaki, akitoa maelezo kuhusu uhakiki wa wastaafu, kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yenye Kaulimbiu kuu “Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania”, yanayofanyika katika viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Maafisa wa Wizara ya Fedha, wakiendelea kutoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yenye Kaulimbiu kuu “Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania”, yanayofanyika katika viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Mwandishi Mwendesha Ofisi Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Bi. Masia Msuya, akimsainisha kitabu cha wageni Mwananchi aliyetembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yenye Kaulimbiu kuu “Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania”, yanayofanyika katika viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Maafisa wa Wizara ya Fedha, wakiwa katika picha ya pamoja katika Banda la Wizara ambapo wameendelea kutoa elimu kwa wananchi wanaotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yenye Kaulimbiu kuu “Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania”, yanayofanyika katika viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF- Dar Es Salaam.)

………….

Na. Saidina Msangi na Asia Singano, WF – Dar Es Salaam

Wizara ya Fedha imebainisha kuwa utekelezaji wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027, utaleta tija kwa wananchi kupitia upatikanaji wa huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo afya na elimu zilizoimarishwa, kurahisisha usafiri na biashara kupitia miundombinu bora, na kufungua milango ya ajira na uwekezaji.

Hayo yalibainishwa na Mchumi Mwandamizi, Wizara ya Fedha, Bi. Consolata Komba, wakati akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayofanyika katika Viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam, yakiwa na Kaulimbiu kuu “Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania”.

Alisema ili kufikia malengo hayo ni jukumu la kila mwananchi kuona bajeti hiyo kama ramani ya maendeleo, na hivyo kushiriki kikamilifu katika uzalishaji, kulipa kodi kwa uaminifu, na kuzichangamkia fursa zilizopo kwa ustawi wa Taifa.
“Bajeti hii ya mwaka 2026/27 ya Shilingi trilioni 62.33 ni ramani thabiti itakayochochea tija katika kilimo, kuimarisha miundombinu, na kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji ili kutengeneza ajira zaidi kwa vijana wetu”, alisema Bi. Consolata.

Alisema bajeti hiyo iliyoidhinishwa na Bunge hivi karibuni, ambayo utekelezaji wake unaanza Julai Mosi 2026, imelenga kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi wa kitaifa, kuboresha miundombinu mbalimbali ya kimkakati, na kuinua ustawi wa kijamii kwa wananchi kote nchini kupitia ugawaji wa kimkakati wa rasilimali za umma.

Bi. Consolata alifafanua kuwa, Serikali imeweka msisitizo mkubwa katika kuongeza uzalishaji kwenye sekta za kimkakati ikiwemo kilimo, mifugo na uvuvi, pamoja na kuimarisha huduma za jamii zikiwemo afya na elimu.

‘‘Bajeti hii pia inalenga kukuza viwanda na uwekezaji, kuimarisha mifumo ya TEHAMA ili kurahisisha utoaji wa huduma za Serikali, kuongeza ukusanyaji wa mapato ya ndani, na kuendelea kulinda makundi maalum katika jamii dhidi ya changamoto za kiuchumi’’, alifafanua Bi. Consolata.

Aidha, Bi Consolata aliwaeleza wananchi majukumu ya Wizara ya Fedha, kupitia Idara ya Bajeti kuwa, ina jukumu la kuratibu maandalizi, utekelezaji na usimamizi wa Bajeti ya Serikali ili kuhakikisha rasilimali za umma zinatumika kwa ufanisi na kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa.