Mkuu wa Wilaya ya Misungwi johari samizi (kulia) akipata maelezo kutoka kwa mmoja wa wazamini wa jukwaa la wataalam wa ununuzi na ugavi lililozinduliiwa rasm jijini mwanza
Na Hellen Mtereko,Mwanza
Wataalam wa ununuzi na ugavi nchini wametakiwa kuzingatia maadili ya kazi, uwajibikaji na matumizi ya teknolojia ili kuongeza ufanisi katika mnyororo wa ugavi na kuchochea maendeleo endelevu ya taifa.
Wito huo umetolewa Jijini Mwanza na kaimu Mkuu wa mkoa wa Mwanza Johari Samizi ambaye ni mkuu wa Wilaya ya Misungwi wakati alipokuwa akifungua rasmi jukwaa hilo la wataalamu wa ununuzi na ugavi lililoandaliwa na Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB).
Samizi, alisema kuwa maendeleo endelevu hayawezi kupatikana bila kuzingatia maadili ya kikazi na uwajibikaji katika sekta ya ununuzi na ugavi.
Alibainisha kuwa zaidi ya asilimia 70 ya bajeti ya taasisi nyingi hutumika katika shughuli za ununuzi, hivyo ni muhimu kwa wataalamu wa sekta hiyo kuhakikisha wanafuata sera, sheria na taratibu zilizowekwa ili kuimarisha uwazi na uadilifu.
“Jukwaa hili litumike kuongeza tija, uwajibikaji na uadilifu katika mnyororo wa ugavi. Pia matumizi ya teknolojia katika shughuli za ununuzi yataongeza uwazi, kasi na ufanisi katika utendaji wa kazi,” alisema Samizi.
Alisema kuwa ushirikiano miongoni mwa wataalamu wa ununuzi na ugavi ni muhimu katika kuongeza ubunifu na kuimarisha utendaji wa sekta hiyo inayochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya uchumi wa nchi.
Vile vile, Ameiagiza PSPTB kuendelea kutoa elimu kwa maofisa ugavi wa Halmashauri nchini ili waweze kutumia mifumo ya kidijitali kwa umakini na ufasaha.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa PSPTB, Godfred Mbanyi alisema jukwaa hilo litaendelea kufanyika kila mwaka kwa lengo la kuwawezesha wataalamu kubadilishana uzoefu, kujifunza mbinu mpya na kujenga mitandao imara ya kitaaluma.
