Chama cha Wafanyakazi wa Ukusanyaji wa Mapato Tanzania (TAREWU) kimeingia makubaliano na BodyMind Insight (BMI) yenye lengo la kuimarisha afya ya akili, ustawi wa kisaikolojia na maendeleo ya wanachama wake.
Makubaliano hayo yalisainiwa katika hafla iliyofanyika katika ofisi za BMI jijini Dar es Salaam, yakifungua ukurasa mpya wa ushirikiano katika masuala ya ustawi wa wafanyakazi.
Akizungumza baada ya utiaji saini huo, Katibu Mkuu wa TAREWU, Dk. Michael Marere, alisema chama hicho kimeamua kuweka mkazo zaidi katika kulinda afya ya akili ya wanachama wake ili kuongeza ufanisi kazini.
Alisema kupitia ushirikiano huo, wanachama watapata elimu na mafunzo yatakayowasaidia kukabiliana na changamoto za maisha na mazingira ya kazi yanayobadilika kwa kasi.
Dk. Marere alieleza kuwa afya ya akili ni nguzo muhimu ya maendeleo ya mfanyakazi na kwamba wafanyakazi wenye ustawi mzuri wa kisaikolojia huongeza tija, ubunifu na uwajibikaji katika kazi zao.
Kwa mujibu wake, hatua hiyo pia itasaidia kujenga ustahimilivu miongoni mwa wafanyakazi na kuchochea maendeleo ya taasisi pamoja na taifa kwa ujumla.
Naye Mkurugenzi wa BMI, John Ambrose, alisema afya ya akili ndiyo msingi wa mafanikio ya mtu binafsi na taasisi, hivyo kuna umuhimu wa kuunda mazingira salama yanayozingatia ustawi wa wafanyakazi.
Ambrose alisema ripoti za afya ya akili mahali pa kazi duniani zinaonyesha ongezeko la changamoto za kisaikolojia, ikiwamo matatizo ya usingizi na shinikizo la madeni na mikopo, hali inayohitaji elimu na hatua za haraka
