Na, mwandishi wetu – Dar es Salaam

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Dkt.Jim Yonazi ameongoza Kikao cha Makatibu Wakuu cha Maandalizi ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) kwa ajili ya kupitia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika maandalizi ya michuano hiyo mikubwa itakayofanyika mwaka 2027 katika nchi za Tanzania, Uganda na Kenya.

Dkt. Yonazi ameongoza kikao hicho leo tarehe 08 Juni, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ndogo ya Waziri Mkuu Magogoni jijini Dar es Salaam.

Ametumia nafasi hiyo kuwasihi wajumbe wa kikao hicho kuendelea kufanya maandalizi kwa weledi huku wakishirikisha sekta zote muhimu katika kufanikisha michuano hiyo na kufikia malengo yanayotarajiwa ili kuipa nchi heshima inayostahili.

“Kila sekta iendelee kutekeleza jukumu lake kwa ufanisi ili kuleta matokeo chanya, “ alisema Dkt. Yonazi

Aidha, Dkt. Yonazi amewashukuru wajumbe wote na kusema kuwa Ofisi yake itaendelea kuratibu shughuli hizo kwa ushirikiano wa pamoja.