Na John Walter -Kondoa
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Wazo Michael Mwang’onda amewataka vijana nchini kuwa wazalendo, wenye nidhamu na kuzingatia maadili mema ili kujenga taifa bora la sasa na la baadaye.
Mwang’onda ametoa rai hiyo alipokuwa akizungumza na wakazi wa Kijiji cha Bukulu, kata ya Soera, Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma mara baada ya Mwenge wa Uhuru kuwasili wilayani humo ukitokea Wilaya ya Bahi.
Amesema vijana wana nafasi kubwa katika maendeleo ya taifa hivyo wanapaswa kujiepusha na vitendo vinavyokiuka maadili, huku wakijikita katika elimu, kazi na uzalendo kwa manufaa ya taifa.
Aidha, amewataka wazazi na walezi nchini kuwalea watoto wao katika misingi ya maadili mema, heshima na uwajibikaji ili kujenga jamii yenye utu na mshikamano.
“Kila mzazi ana wajibu wa kuhakikisha watoto wanakuwa katika maadili mema kwani hiyo ndiyo njia ya kujenga taifa lenye heshima na maendeleo endelevu,” amesema Mwang’onda.
Kauli mbiu ya Mwenge wa Uhuru mwaka 2026 inasema; “Tanzania ni yetu sote, tushikamane kwa pamoja kuleta maendeleo.”

