Wizara ya Maji ni miongoni mwa washiriki wa Maadhimisho ya Wiki ya Mazingira Kitaifa yanayofanyika katika viwanja vya ukumbi wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma.

Maadhimisho yamebeba kauli mbiu isemayo: “Dira 2050 Tuwajibike kukijanisha Tanzania”

Wiki ya Mazingira Kitaifa na yatafanyika kuanzia tarehe 1-5 Juni,2026.

Kila mwaka maadhimisho haya huwakutanisha wadau kutoka sekta mbalimbali za Serikali na binafsi kwa lengo la kujadili na kuonesha jitihada zinazofanyika katika kuhifadhi mazingira na kuhakikisha matumizi endelevu ya rasilimali za taifa.

Wakati wa ufunguzi wa Maadhimisho hayo, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Reuben Kwagilwa (Mb) amesisitiza uhifadhi wa mazingira kuwa sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 kwa kupanda miti kwa kiwango kikubwa zaidi nchini, kupunguza uchafuzi wa mazingira na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuimarisha biashara ya kaboni na miradi ya kijani.

“Tunapaswa kulinda mazingira yetu kwa wivu mkubwa kwani ndio rasilimali iliyobeba uhai wa viumbehai pia napenda kumshukuru Rais Mhe. Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuruhusu mswada wa sheria mpya ya mazingira kupitiwa bungeni hii itaongeza chachu katika mapambano ya utunzaji wa mazingira” amesema Mhe. Kwagilwa

Wizara ya Maji imehusisha taasisi zake kama ikiwamo DUWASA, DAWASA, RUWASA na Mfuko wa Taifa wa Maji ambapo elimu inatolewa kwa wananchi kuhusu huduma za majisafi na usafi wa mazingira, uhifadhi wa vyanzo vya maji, pamoja na juhudi mbalimbali zinazotekelezwa na Wizara ya Maji na Taasisi zake katika kuboresha upatikanaji wa huduma za maji kwa wananchi.