Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake wa Kiislamu Tanzania (JUWAKITA) Mkoa wa Mwanza, Amina Masenza, amewataka wazazi na walezi kushiriki kikamilifu katika mijadala ya malezi ya watoto ili kusaidia kukabiliana na changamoto ya mmomonyoko wa maadili unaoendelea kujitokeza katika jamii.
Amesema ushiriki wa wazazi katika malezi bora ni msingi muhimu wa kujenga taifa lenye vijana wenye maadili na nidhamu.
Akizungumza jijini Mwanza baada ya hafla ya chakula kwa watoto yatima iliyoandaliwa kwa ushirikiano wa BAKWATA Mkoa wa Mwanza na Rocky Solution, Masenza alisema wazazi wanapaswa kuhakikisha watoto wanalelewa katika mazingira yatakayowajenga kiimani, kimaadili na kijamii.
Alisema kasi ya utandawazi imeleta changamoto mpya zinazohitaji malezi ya karibu zaidi kutoka kwa wazazi na walezi.
Masenza alisema vijana wanapaswa kuelekezwa kuchagua mambo yenye manufaa kwa maisha yao na kuepuka mambo ya ovyo ya shetani na tabia zinazoweza kuharibu mustakabali wao kimaisha.
Aliongeza kuwa pamoja na faida zilizopo katika maendeleo ya teknolojia na utandawazi, bado yapo mambo yanayochochea kuporomoka kwa maadili, hivyo jamii ina wajibu wa kuwaongoza watoto katika misingi bora ya maisha l vijana wachague mambo mazuri ya kuwafaa.
Kwa upande wake, Sheikh Hassani Kabeke aliwahimiza waumini wa Kiislamu kurejea katika misingi ya dini kwa kuwalea watoto yatima kwa upendo na huruma badala ya kuwachukulia kama wafanyakazi wa majumbani.
Alisema kuwalea watoto yatima ni jambo lenye thawabu kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu na jamii inapaswa kurejesha utamaduni wa kusaidiana katika malezi ya watoto hao.
Aidha, Sheikh Kabeke alivipongeza vyombo vya ulinzi na usalama kwa juhudi zao za kudhibiti vitendo vya ukatili dhidi ya watu wenye ualbino, hali iliyosaidia kundi hilo kuendelea kuishi kwa amani na kufanya shughuli zao kwa uhuru.
Alitoa rai kwa Watanzania kuendelea kupinga vitendo vya unyanyapaa na ukatili dhidi ya watu wenye ualbino ili kudumisha mshikamano, utu na amani katika jamii.

