Na Mwandishi Wetu,Mbinga
MRAJISI Msaidizi wa vyama vya ushirika mkoani Ruvuma Venance Msafiri,amezindua matumizi ya mizani za kidijitali zilizounganishwa na mfumo wa usimamizi wa vyama vya ushirika(MUVI)utakaoimarisha utendaji na kuimarisha vyama vya ushirika mkoani humo.
Msafiri amesema,sasa ni zama za kidijitali hivyo vyama vyote vya ushirika wa mazao mkoani Ruvuma vina wajibu wa kutumia mizani zilizounganishwa na mfumo wa upimaji wa mazao katika kutekeleza majukumu yao ya kukusanya na kuuza mazao ya wakulima hususani yale yaliyoingizwa kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani.
Msafiri amesema hayo jana wilayani Mbinga,wakati akifunga mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo wa matumizi sahihi ya mizani za kidijitali mameneja na makarani wa vyama vya msingi vya ushirika(Amcos)wilayani Mbinga.
Msafiri,amesisitiza viongozi na watendaji wote wa vyama vya msingi vya ushirika wa mazao Mkoani Ruvuma wahakikishe wanasimamia matumizi sahihi ya vipimo na mizani za kidijitali zilizohakikiwa na wakala wa vipimo nchini.
Aidha,amewataka watendaji hao kuanza kukusanya kahawa kwa wakulima,kusimamia ubora wa kahawa zinazoletwa na wakulima na kurejesha fedha za ukomo wa madeni zilizopelekwa kwenye vyama vyao kwa ajili ya kukusanya kahawa.
Pia,ametoa muda wa wiki moja kwa viongozi hao wa Amcos kurudisha mizani za zamani zilizopigwa marufuku na Serikali ambazo kwa muda mrefu zimekuwa zinalalamikiwa na wakulima.
“ndugu zangu kahawa bado inahitajika sana Duniani,kwa hiyo nawaomba twendeni tukaendelee kuzalisha na tukasimamie ubora wa kahawa zinazoletwa na wakulima wetu kwani kahawa ya Mbinga imekuwa ikipata sifa kubwa kutokana na ubora wake”alisema Msafiri.
Meneja wa Chama kikuu cha ushirika wa mazao wilayani Mbinga(Mbifacu)Faraja Komba alisema,lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo watendaji wa Amcos wa kutumia mizani za kidijitali ili kurahisisha shughuli za upimaji wa mazao ya wakulima kwenye vyama vyao.
Alisema,matumizi sahihi ya mifumo iliyounganishwa na mizani za kidijitali kwa kiwango zinatoa uwazi hivyo, zitasaidia kupunguza malalamiko ya wakulima kupunywa kiasi cha mazao wanayopeleka kwenye vyama vya ushirika,kuwezesha upatikanaji wa taarifa na takwimu sahihi kwani zinatoa lisiti kulingana na mzigo ulioletwa na mkulima.
Alisema hadi sasa,wamepokea jumla ya mizani 300 kutoka kwa kampuni ya Climb up Ltd ambazo zinaendelea kusambazwa kwenye vyama vya msingi vya ushirika ambapo mizani 118 zimepelekwa kwenye vyama hivyo na vyama vinaendelea kuongeza kulingana na idadi ya vituo vya kupima kahawa.
Komba alisema,Mbifacu inasimamia jumla ya Amcos 129 katika mkoa wa Ruvuma,hata hivyo viongozi waliohudhuria mafunzo hayo ni kutoka Amcos 107 na 18 hawakuhudhuria ambapo kwa upande wa wilaya ya Nyasa Amcos 3 hazijahudhuria,Mbinga Mji Amcos 4 na Mbinga vijijini 10.
Kwa upande wake Afisa ushirika wa wilaya ya Nyasa Menance Ndomba alisema,mafunzo hayo yamebeba dhana moja ya uwadilifu kwa viongozi wa vyama vya ushirika kwani kwa kutumia mizani za kidijitali sasa viongozi hao wameongezewa nguvu na kuaminiwa zaidi na wakulima kama watatumia ipasavyo mizani hizo.
“wengi wanaamini kwa kutumia kalamu kwa kuandika listi ndipo kuna nafasi ya kufanya udanganyifu,sasa kwa kuwa takwimu zote zitaendena na mizani hizi na listi zitakazotoka zitamwanisha mwanachama wa chama chako kwamba uadilifu umefikia kiwango kinachotosheleza”alisema Ndomba.

