Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, akipokea zawadi maalum kutoka kwa Meneja wa Biashara Zanzibar wa Benki ya NMB, Bi. Naima Said Shaame, wakati wa Mkutano wa Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Bodi wa Taasisi za Kizanzibari uliofanyika Golden Tulip Airport Hotel, Zanzibar. Kushoto ni Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa NMB, Bi. Vicky Bishubo. Zawadi hiyo ilitolewa kama ishara ya kuthamini uongozi wa Rais Dkt. Mwinyi katika kukuza uchumi wa Zanzibar na kuimarisha mazingira wezeshi kwa biashara na uwekezaji.
………..
Zanzibar. Benki ya NMB imesema itaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na taasisi zake katika kuimarisha mifumo ya malipo, makusanyo, huduma za kidijitali na suluhisho za kifedha zinazolenga kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi na wawekezaji.
Kauli hiyo imetolewa wakati wa Mkutano wa Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Bodi wa Taasisi za Kizanzibari unaofanyika Golden Tulip Airport Hotel, Zanzibar, kuanzia Mei 23 hadi 25, 2026, ambapo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, aliwataka viongozi wa taasisi hizo kuleta mageuzi ya kiutendaji yatakayoongeza tija, kupunguza utegemezi kwa Serikali Kuu na kuwezesha taasisi kutoa gawio kwa Serikali.
Akifungua mkutano huo, Rais Dkt. Mwinyi alisema kasi ya maendeleo itaongezeka zaidi kupitia ushirikiano imara na sekta binafsi, akitolea mfano mabenki yanayofanya vizuri nchini kwa kuonyesha ukuaji mkubwa, faida nzuri na kutoa gawio kubwa kwa Serikali.
“Taasisi zetu zinapaswa kujifunza kutoka kwenye mifano mizuri ya sekta binafsi, hasa mabenki binafsi yanayoonyesha ufanisi, faida na mchango mkubwa wa gawio kwa Serikali,” alisema Dkt. Mwinyi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa NMB, Bi. Vicky Bishubo, alisema NMB inaona Zanzibar kama mshirika muhimu katika ajenda ya maendeleo kupitia uwekezaji, uchumi wa bluu, utalii, biashara, teknolojia na huduma za kifedha. Alisema NMB tayari inashirikiana na EGAZ, ZIPA na taasisi nyingine za Zanzibar katika kuboresha huduma za kidijitali, uwekezaji na uhifadhi wa maeneo ya kimkakati, huku pia ikitoa mafunzo kwa zaidi ya wajasiriamali 10,000 wa Zanzibar wanaojihusisha na mwani, chumvi na uvuvi.

