Na Mwamvua Mwinyi-Rufiji Mei 24,2026

Halmashauri ya Mji Rufiji kuanzisha mfumo wa utoaji tuzo kwa kata zitakazofanya vizuri katika usimamizi wa shughuli za maendeleo pamoja na ukusanyaji wa mapato kupitia kadi maalum ya kupima utendaji kazi (score card) , kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26, Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Simon Berege alisema mfumo huo unalenga kuongeza uwajibikaji, ushindani chanya na ufanisi katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo kuanzia ngazi za chini .

Ameeleza miongoni mwa maeneo yatakayopimwa ni ukusanyaji wa mapato, utekelezaji wa miradi ya maendeleo, utatuzi wa kero za wananchi, udhibiti wa mimba za utotoni, huduma za afya, lishe na maeneo ya kijamii.

Kwa mujibu wa Berege, mshindi wa jumla atapatiwa tuzo maalum huku kata itakayofanya vibaya zaidi itapewa “zawadi ya kushindwa” kwa lengo la kuhamasisha uwajibikaji na kujitathmini.

Vilevile, alieleza tuzo hizo zitawahusisha watendaji wa kata, wasimamizi wa sekta mbalimbali na madiwani ili kuongeza ari ya kusimamia maendeleo ya wananchi.