Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Norway nchini Tanzania, Mhe. Tone Tinnes yaliyolenga kuimarisha na kuendeleza ushirikiano kati ya nchi hizo mbili katika sekta ya nishati.
Mazungumzo hayo yamefanyika leo Mei 22, 2026 katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Nishati zilizopo jijini Dar es Salaam.
Viongozi hao wamejadili masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya nishati ikiwemo mashirikiano ya kimkakati katika uendelezaji wa gesi, umeme, nishati jadidifu pamoja na kubadilishana uzoefu wa kitaalamu na juhudi za kukuza sekta ya nishati kwa nchi hizo mbili.
Kikao hicho kimehudhuriwa pia na Kamishna wa Mafuta na Gesi kutoka wizara ya nishati, Bw. Goodluck Shirima, Mkurugenzi wa Maendeleo na Uzalishaji kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Bw. Paschal Njiko pamoja na wataalamu wengine.

