Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Mali za Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Chotto Sendo, akizungumza kwa niaba ya Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Bw. Nsubili Joshua, wakati akifungua mafunzo kwa Menejimenti ya Wizara kuhusu Mwongozo wa Udhibiti wa Ndani wa Wizara ya Fedha, yaliyofanyika katika Hotel ya Morena mkoani Morogoro.

Na. Chedaiwe Msuya, WF, Morogoro

Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Bw. Nsubili Joshua, amekiagiza Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini cha Wizara ya Fedha kuratibu ujenzi wa mchakato wa utekelezaji wa majukumu (business processes) za kidigitali ili kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa majukumu ya Wizara.

Maagizo hayo yametolewa kwa niaba yake na Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Mali za Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Chotto Sendo, wakati akifungua mafunzo mafunzo ya Mwongozo wa Udhibiti wa Ndani wa Wizara ya Fedha, kwa

Menejimenti ya Wizara hiyo, yaliyofanyika katika Hotel ya Morena mkoani Morogoro.

Alisema business processes mpya zinazotakiwa ni pamoja na ufuatiliaji wa Mfumo wa Ununuzi (NeST), ufuatiliaji na udhibiti wa mapato kupitia big data analysis, ufuatiliaji wa miradi ya PPP, miradi ya alternative financing, ulipaji wa michango ya Serikali kwenye taasisi za kimataifa, na ufuatiliaji wa mapato yasiyo ya kodi.

Aidha, Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini (M&E) kimetakiwa kuhakikisha kuwa business processes hizo zinajengwa kwa mfumo wa kielektroniki ili kurahisisha ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara ili kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ufanisi wa mifumo ya kiutendaji.

Bw. Sendo, alifafanua kuwa mafunzo hayo yataiwezesha Menejimenti na Watumishi wa Wizara kuelewa dhana na mbinu za udhibiti wa ndani, kujifunza namna ya kuchambua viashiria hatarishi, na kuimarisha business processes zilizopo.

“Mwongozo huu utakuwa na manufaa makubwa ikiwemo kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji na tathmini kwa njia za kidigitali, kuwezesha Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani kufanya tathmini kwa mujibu wa Mwongozo wa Kimataifa wa Ukaguzi wa Ndani wa mwaka 2024, na kuweka vigezo vya kupima ufanisi wa mifumo ya kiutendaji”, alisisitiza Bw. Sendo.

Aliwasisitiza washiriki wa mafunzo hayo kufuatilia kwa umakini ili kuutumia Mwongozo huo kuboresha mfumo wa udhibiti wa ndani katika maeneo yao ya kazi ili kuimarisha uchumi wa taifa kupitia usimamizi bora wa rasilimali za umma.

Naye Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Kenneth Nindie, alitoa rai kwa Idara zote za Serikali kuhakikisha wanatumia vizuri Mwongozo huo ili uweze kuwasaidia kuweka taratibu vizuri na malengo ya Wizara yanafikiwa kwa ufasaha.

Kwa upande wake, Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali Msaidizi Bw. Abraham Msechu, amesema kuwa mafunzo yatasaidia Menejimenti ya Wizara kupata uelewa wa Mwongozo wa Udhibiti wa Ndani na kuimarisha mifumo ya udhibiti wa ndani.

Akizungumzia mafunzo hayo mmoja wa washiriki, Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama, aliahidi kuyafanyia kazi mafunzo yote waliyopata katika Idara na Vitengo ili kufikia malengo ya Serikali katika udhibiti wa ndani.

Mafunzo hayo yamewajumuisha Menejimenti ya Wizara ya Fedha pamoja na Watumishi wa Wizara na Wawezeshaji kutoka Kampuni ya Ushauri (KPMG).