*†Hajaridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mkandarasi kwenye mradi
*Aagiza ukaguzi maalum wa matumizi ya dola milioni 20 za malipo ya awali yaliyotolewa kwa mkandarasi kulinganisha na kazi zilizofanyika
*Aelekeza kuondolewa mara moja kwa meneja wa mradi upande wa mkandarasi
Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi amesema hajaridhishwa na mwenendo wa utekelezaji wa Mradi wa Kuzalisha Umeme wa Megawati 49.5 katika maporomoko ya Mto Malagarasi mkoani Kigoma unaotekelezwa na Kampuni ya Dongfang Electric kutokana na kuchelewa kwa kazi pamoja na kutotekeleza masharti ya mkataba waliouingia na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).
Mhe. Ndejembi ametoa kauli hiyo Mei 10, 2026 wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya mradi huo ambapo alibaini mkandarasi huyo amekuwa akitoa visingizio badala ya kutekeleza majukumu yake kwa wakati kama mkataba unavyoelekeza.
Akizungumza katika ziara hiyo, amesema Serikali tayari imemlipa mkandarasi zaidi ya dola milioni 20 kama malipo ya awali lakini kiwango cha kazi zilizotekelezwa hakionekani kuendana na fedha zilizotolewa.
Baadhi ya kazi zilizochelewa ni pamoja na ujenzi wa makazi ya wafanyakazi na barabara za mradi, hali ambayo imeonesha kusuasua kwa utekelezaji wa mradi huo wa kimkakati.
Aidha, ameielekeza TANESCO pamoja na mshauri mwelekezi kuendelea kumsimamia kwa karibu mkandarasi huyo huku akisisitiza kuwa Serikali haitatoa nyongeza ya fedha wala kuruhusu mabadiliko ya gharama za mradi huo kwani mkandarasi aliwasilisha gharama zake mwenyewe wakati wa zabuni.
Amesema baadhi ya wakandarasi wamekuwa na tabia ya kuomba kazi kwa gharama ndogo ili kupata zabuni na baadaye kuanza kuomba nyongeza ya fedha, jambo ambalo Serikali haitalivumilia.
Katika hatua nyingine, Mhe. Ndejembi ameagiza meneja wa mradi upande wa mkandarasi kuondolewa mara moja kutokana na kile alichokieleza kuwa ni visingizio vinavyochangia kuchelewesha utekelezaji wa kazi.
Vilevile ameagiza kufanyika kwa ukaguzi maalum wa matumizi ya fedha za malipo ya awali ili kubaini namna fedha hizo zimetumika ukilinganisha na kazi zilizofanyika.
“Mradi huu una umuhimu mkubwa kwa wananchi wa Kigoma, Katavi, Kagera na maeneo ya jirani kwani utaongeza nguvu katika Gridi ya Taifa na kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika nchini. Serikali haitakuwa tayari kuvumilia ucheleweshaji unaosababishwa na uzembe wa wakandarasi,” amesema Mhe. Ndejembi.
Ameielekeza TANESCO ndani ya muda wa wiki mbili kukamilisha ukaguzi huo na kuwasilisha taarifa ofisini kwake.
Aidha, amempongeza Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO kwa juhudi za kufanya vikao vya mara kwa mara na mkandarasi huyo pamoja na kuchukua hatua mbalimbali za kutatua changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa mradi.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa TANESCO Bw, Lazaro Twange amesema TANESCO imepokea maelekezo yote yaliyotolewa na Waziri na itahakikisha yanatekelezwa kwa wakati ili mradi huo ukamilike kama ilivyopangwa.
Mradi wa Malagarasi MW 49.5 unatekelezwa na Kampuni ya Dangfang Electric International Corporation (DEC) kutoka China, ambapo ulianza Aprili 30, 2024 na unatarajiwa kukamilika Oktoba 30, 2027 kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 300.
Kukamilika kwake kutaimarisha hali ya upatikanaji wa umeme
Katika mikoa ya Kigoma, Katavi, Kagera na maeneo ya jirani kwani utaongeza nguvu katika Gridi ya Taifa.

