8 May 2026, 7:04 pm
Wanaume wakazi wa kata ya Nyanguku manispaa ya Geita wakiwa katika eneo la mradi wa kisima. Picha na Ester Mabula
………..
“Huu ni mwaka wa nne tangu huu mradi uanze na kila siku tumekuwa tukipewa ahadi tu kila kiongozi anayekuja anasema utakamilika, tunaomba mamlaka zitusaidie” – Mwananchi wa Nyanguku
Na: Ester Mabula
Wakazi wa kata ya Nyanguku iliyopo halmashauri ya manispaa ya Geita wameiomba serikali kuwasaidia kukamilisha mradi wa ujenzi kisima cha maji ambao umekwama kwa zaidi ya miaka minne hali inayopelekea wananchi kutembea umbali mrefu kufuata maji katika maeneo jirani.
Wakizungumza na waandishi wa habari wameeleza wamekuwa wakipewa ahadi za mara kwa mara za kukamilisha mradi huo lakini hadi sasa hakuna kinachoendelea.
Diwani wa kata ya Nyanguku ambaye pia ni Naibu Meya Elias Ngole akizungumza katika kikao cha baraza la madiwani. Picha na Ester Mabula
Mei 07, katika kikao cha baraza la madiwani manispaa ya Geita Diwani wa kata hiyo Elias Ngole ambaye pia ni Naibu Meya wa manispaa ya Geita aliibua hoja na kutaka majibu ya uhakika kutoka GEUWASA juu ya lini mradi huo utakamilika huku akihoji sababu ya kukwama kwa mradi huo.
Akijibu hoja ya Diwani wa kata hiyo, Mhandisi kutoka GEUWASA Yohanna Masheria amesema kinachokwamisha mradi huo ni fedha za kuwalipa wazabuni huku akiahidi kufatilia changamoto hiyo.
