Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), ameagana na Balozi mteule wa Tanzania katika Jamhuri ya Korea Mhe. Balozi Noel E. Kaganda.
Akizungumza katika kikao hicho kilichofanyika tarehe 30 Aprili, 2026 katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam, Waziri Kombo amemsii Balozi Kaganda kuendeleza ushirikiano wa kimkakati uliopo baina ya Tanzania na Jamhuri ya Korea, hususan katika sekta za uchumi wa buluu, elimu, miundombinu, teknolojia, viwanda, biashara, uwekezaji, afya na utalii.
Aidha, amemsisitiza kufuatilia utekelezaji wa makubaliano yote yaliyofikiwa baina ya nchi hizi mbili, ikiwemo utekelezaji wa miradi iliyosainiwa wakati wa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, mwezi Juni 2024.
Kwa upande wake, Balozi Kaganda amemshukuru Waziri Kombo kwa nasaha na miongozo yake na kuahidi kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa vitendo kwa maslahi ya taifa.
Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara, Balozi Dkt. Samwel W. Shelukindo, ambaye aliungana na Waziri Kombo kumtakia Balozi Kaganda uwakilishi mwema huko Seoul, Jamhuri ya Korea.





