Uwekezaji huo, unatarajiwa kufanyika kupitia miradi ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) na utazingatia vipaumbele vya maendeleo ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan na utatekezwa kwa awamu mbalimbali.
Waziri Mkumbo aliipongeza SinoAm LLC kwa kuonesha dhamira ya dhati ya kuwekeza kiasi kikubwa cha mitaji nchini Tanzania, akibainisha kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wakubwa wa kimataifa.
“Tanzania ina utulivu wa kisiasa, sera rafiki za uwekezaji, na dira ya muda mrefu ya maendeleo inayotoa uhakika na ulinzi kwa uwekezaji wa kimkakati” Alisema Prof. Mkumbo.
Kwa upande wake Bw. Najib Choufani, Mwenyekiti wa Mfuko huo, alibainisha kuwa SinoAm LLC imefanya tathmini ya kina ya mazingira ya uwekezaji nchini Tanzania na kubaini fursa zenye tija kubwa, ikiwemo ujenzi na uendeshaji wa barabara za kisasa za kulipia (toll expressways).
Aidha, miradi ya reli ya kiwango cha kimataifa (SGR), pamoja na miundombinu muhimu ya uchukuzi na nishati inayochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ushindani wa Tanzania kikanda ni miongo mwa maeneo yanayolengwa.
Katika mkutano huo, Mhe. Waziri ameambatana na Katibu Mkuu Dkt. Tausi M. Kida, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo maalumu ya Kiuchumi TISEZA Bw. Giread Teri, huku uongozi wa SinoAm LLC pia uliambatana na Bw. Tarek Choufani, Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko huo, ambaye alieleza kuwa SinoAm ina uzoefu mpana wa kimataifa katika kusimamia miradi mikubwa ya miundombinu na iko tayari kuleta si tu mitaji mikubwa, bali pia utaalamu wa kiufundi, mifumo ya kisasa ya usimamizi na mbinu bora za kimataifa nchini Tanzania.




