Na John Walter -Manyara.
Serikali imepanga kupeleka shilingi bilioni 335.6 kwa mwaka wa fedha 2025/2026 ili kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika mkoa wa Manyara.
Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, alitoa taarifa hiyo akiwa Kijiji cha Muungano, Kata ya Laghanga, Wilaya ya Hanang’ wakati akianza ziara ya siku nne wilayani humo.
Lengo la ziara hiyo ni kuwaeleza wananchi maendeleo yaliyofanyika mkoani humo katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Mhe. Sendiga alieleza kuwa bajeti hiyo ilipitishwa katika kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kilichofanyika Machi 24, 2025, jijini Dodoma, ambapo wakuu wa mikoa walihudhuria.
Hata hivyo, bajeti hiyo inasubiri kupitishwa rasmi na Bunge kabla ya kuanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha wa serikali.
Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa fedha hizo zinatumika kuboresha huduma za jamii na kuleta maendeleo kwa wananchi wa Manyara, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ustawi wa mkoa huo chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.