Afisa Mtendaji  wa Kata  ya Dung’unyi wilayani, Ikungi mkoani Singida  Yahaya Njiku, akizungumza na Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Munkinya wakati wa ziara yake ya kukagua miradi katika  kata hiyo aliyoifanya jana ambapo pia alipata fursa ya kuzungumza na Wazazi na Walezi wa wanafunzi hao.
Afisa Mtendaji  wa Kata  ya Dung’unyi wilayani, Ikungi mkoani Singida  Yahaya Njiku, akisisitiza jambo wakati akizungumza na wanafunzi hao.
Wazazi na Walezi wakiwa kwenye mkutano huo.
Afisa Elimu wa Kata ya Dung;unyi, Ester Mkoma (kushoto) akizungumza na Wazazi na Walezi katika ziara hiyo.
Afisa Mtendaji  wa Kata  ya Dung’unyi wilayani, Ikungi mkoani Singida  Yahaya Njiku, akizungumza na Wazazi.
Afisa Mtendaji  wa Kata  ya Dung’unyi wilayani, Ikungi mkoani Singida  Yahaya Njiku, akizungumza na Wanafunzi wa shule hiyo. 

 

Na Dotto Mwaibale, Singida

 

AFISA Mtendaji wa Kata  ya
Dung’unyi wilayani, Ikungi mkoani Singida  Yahaya Njiku ametoa onyo kali
kwa Wazazi na Walezi wenye tabia ya kuwarubuni watoto wao waache kwenda shuleni
huku wakitoa sababu mbalimbali ikiwemo ya kutaka kuwaoza.
 

Njiku alitoa onyo hilo jana
alipokuwa akizungumza na wazazi na wanafunzi  wakati wa ziara yake ya
kukagua miradi katika Shule ya Sekondari Munkinya ilioyopo katika kata hiyo.
 

” Hivi karibuni kumezuka tabia
ya  baadhi ya wazazi kuwarubuni watoto wao waache shule ili wabaki
nyumbani kufanya kazi mbalimbali ikiwemo kuwaoza  na wengine wanaambatana
na watoto wao mpaka ofisi za Serikali za Vijiji na kata ambako wamekuwa wakitoa
madai eti watoto wao hawataki shule hivyo wanaomba wafutwe” alisema Njiku.
 

Njiku alisema mzazi au mlezi atakaye
bainika akifanya hivyo hatamvumilia atamkamata na kumfikisha kwenye vyombo cha
dola na katika jambo hilo hata kuwa na huruma na mtu.

Alisema ni jambo la ajabu kwa mzazi
na mlezi kufanya jambo hilo kwani Serikali imetumia fedha nyingi kuboresha
miundombinu mashuleni ili watoto wapate elimu katika mazingira bora alafu
anatokea mzazi akidai anataka mtoto wake aachishwe shule.
 

” Itakuwa Serikali ya ajabu
ambayo itaukubali upuuzi huo nasema ole wake  mzazi tukakaye mbaini
akifanya hivyo” alisisitiza Njiku kwa ukali.
 

 Alisema ni wajibu wa wazazi na
walezi kushirikiana na Serikali kuhakikisha watoto wanapata mazingira bora ya
elimu wawapo shuleni na nyumbani lakini si kwa kuwarubuni kuacha shule.
 

Njiku alitumia nafasi hiyo
kumshukuru  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassani
kwa kuwapatia kiasi cha Sh. Milion 40 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa mawili
katika shule hiyo ambapo aliwasisitiza 
wanafunzi hao kusoma kwa bidii.