……………………………………………………..

Na Mwandishi Wetu

Mbunge wa Viti Maalumu  anayewakilisha Mkoa wa Dar es Salaam, Janeth Mahawanga, ameshauri vikundi vya wajasiriamali  kuwekeza katika kupata elimu zaidi na teknolojia  ili  kupata tija.

Ameyasema hayo, wakati akifungua kongamano la Vijana na Ujasiriamali  liloandaliwa na Taasisi ya  Tuamke Pamoja Tanzania, katika Jimbo la Ukonga, Dar es Salaam.

Mbunge Janeth alisema, suala la mitaji  si changamoto tena  kwa  wajasiriamali kwani serikali  inatoa mikopo  isiyo na riba  kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu  wenye ulemavu  kupitia  gawio la    asilimia 10 linalotokana na mapato ya ndani ya halmashauri.

“Kikubwa  wajasiriamali wekezeni katika kujifunza. Mshirikini katika mafunzo ili mtambue fursa,”alieleza  Mbunge huyo.

Amebainisha, pia  wajasiriamali wawekeze katika Teknolojia  ambayo ndiyo msingi mkubwa katika kufikia tija kwa sasa.

“Kijana mjasiriamali unamiliki simu janja.  Jiulize unaitumiaje simu hiyo katika kukuletea fursa? Pia ni lazima uwe na juhudi maarifa na uthubu,”alisema  Mahawanga.

Alisema   katika suala la uwezeshaji , vijana wanawake na watu wenye ulemavu mkoani  Dar es Salaam, anamatarajio makubwa ya kuona matokeo chanya ili  kuendana na kasi ya  Rais Samia Suluhu Hassan katika kuleta maendeleo.

Aliwataka  wajasiriamili popote walipo kuwasiliana naye ili kusaidiana katika kufanikisha uundwaji wa vikundi, usajili wa  hata kunapokuwa na mkwamo wa kupata mikopo.

“Kazi yangu mimi siyo kwenda tu Dodoma. Kazi yangu ni kuwatumikieni nyinyi wananchi. Niiteni mtaani kwenu.  Siyo lazima katika ukumbi hata kwenye mikeka tutakaa. Tujadili masuala ya ujasiriamali. Nataka kuona Dar es Salaam, ikifanikiwa katika hili,”alieleza.

Awali Mkurugenzi wa Taasisi ya  Tuamke Pamoja Tanzania, Nasra Msofe, alisema taasisi hiyo inahudumia vikundi nane vya ujasiriamali na imejikita kutoa elimu ya ujasiriamali kwa vijana pamoja na kujitambua.

“Tunataka kuendana na sera ya serikali yetu chini ya Rais Samia ya Uchumi wa Viwanda, hivyo tumejikita katika kuhamasisha jamii    kufanya ujasiriamali na kutafuta masoko ya biashara ,”alieleza.