Na Mwandishi Wetu
Afisa Elimu wa Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi, Jafarani Mapua ameipongeza Menejimenti ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kuona umuhimu wa kufanya uzinduzi wa kampeni ya kuhamasisha mabinti wa Wilaya hiyo kupenda masomo ya sayansi kwani ni heshima ya pekee kwao.
Akizungumza kwenye uzinduzi wa kampeni hiyo, Mapua amesema kampeni hiyo imelenga kuhamasisha na kishawishi wanafunzi wa kike kusoma masomo ya Sayansi na kuongeza udahili wa wanawake wanaosoma masomo hayo ambao kwa muda mrefu umekuwa chini sana.
Aidha, amesema kwa kampeni hiyo inayotarajia kufanyika mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma, Njombe, Mbeya na Iringa kwa kiasi kikubwa utahamasisha na kubadilisha mtazamo wa wanafunzi wa kike kuona masomo ya Sayansi si kwa wanafunzi wa kiume pekee.
“Kwa kuwa sasa Taifa leo linaelekea kwenye uchumi wa viwanda, hivyo tutumie fursa hii kuwahamasisha mabinti zetu waone fursa zilizopo mbele yao ni nyingi katika kukuza uchumi wa viwanda, jitihada zenu katika masomo zitawapa nafasi kubwa katika soko la ajira katika Sayansi, Teknolojia na uhandisi ambazo ndio chachu kuu ya kufikia Tanzania ya viwanda,” amesema.
Mapua amesema mabinti wa wilaya hiyo wamepata bahati kubwa kukutana na wanasayansi wa DIT, ujio wao una chachu kwao kubadilishana mtazamo juu ya masomo ya Sayansi na kuyaona kama masomo mengine na kuongeza bidii ili watengeneze wanasayansi na wahandisi wengi wanawake.
“Naishukuru kwa mara nyingine DIT kwa kuona umuhimu wa wilaya yetu, kuzindua kampeni hizi, jitihada zenu si bure zitasaidia kuzalisha wanasayansi wanawake wengi ambao wataweza kutatua changamoto mbalimbali katika jamii ya watanzania,” amesema Mapua.




—