*******************************
Tarehe 08.07.2021 muda wa 07:00 mchana huko maeneo ya Sombetini katika Jiji la Arusha, Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha lilimkamata na linaendelea kumhoji mganga wa kienyeji (jina limehifadhiwa) mkazi wa Sombetini jijini Arusha kwa tuhuma za kumshawishi mtuhumiwa wa tukio la ukatili dhidi ya Mtoto lililotokea tarehe 06 Julai mwaka huu eneo la Burka. Kama mnavyokumbuka tarehe 08 Julai mwaka huu tulitoa taarifa ya mtoto wa kiume mwenye miaka (4) ambaye alifanyiwa ukatili wa kipigo pamoja na kuwekewa majani mdomoni na baba yake wa kufikia na kutekelezwa katika eneo la Burka.
Katika uchunguzi wetu tumeweza kumhoji mganga huyo wa kienyeji mkazi wa sombetini ambaye amekiri kumshawishi mtuhumiwa huyo aliyemfanyia ukatili mtoto wa miaka minne (04) ambapo alimshawishi kwamba ukifanya kitendo hicho kitamsaidia katika kesi zake pamoja na utajiri katika biashara zake. Jeshi la Polisi linaendelea na Upelelezi pindi utakapokamilika Jalada litapelekwa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka kwa hatua za kisheria.
TAARIFA YA KUSHIKILIWA ASKARI WA JESHI LA WANANCHI WA TANZANIA
Ndugu wanahabari Katika hatua nyingine Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha linamshikilia askari wa Jeshi la wananchi wa Tanzania katika wilaya ya Monduli kwa tuhuma ya mauaji ya LAISI S/O LEMOMO (26) Mfugaji mkazi wa kijiji cha Lashaine wilaya ya Monduli Mkoa wa Arusha.
Tukio lililotokea tarehe 12.07.2021 muda wa 10:00 Jioni huko katika kijiji cha Lashaine wilaya ya Monduli Mkoa wa Arusha, aidha katika kubaini undani wa tukio hilo timu ya makachero imefika eneo la tukio na inaendelea uchunguzi wa tukio hilo na pindi Upelelezi utakapokamilika taarifa zaidi zitatolewa kamilika itatolewa.
Natoa wito kwa Wananchi kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi za waganga wa kienyeji wanaojihusisha na vitendo vya udanganyifu ikiwa ni pamoja na kuwashawishi watu kufanya vitendo vya ukatili dhidi ya kina mama na watoto,kwamba wakifanya hivyo watafanikiwa katika mambo yao mbalimbali.