Meneja wa shirika la Tanesco Mkoa wa Manyara mhandisi Rehema Mashinji akizungungumza na waandishi wa habari Mjini Babati baada ya nguzo 520 kufikishwa eneo hilo na kampuni ya kizalendo ya Qwihaya General ya Wilayani Mufindi Mkoani Iringa.
……………………………………………………………………….
Na Mwandishi wetu, Babati
KAMPUNI ya Qwihaya General ya Wilayani Mufindi Mkoani Iringa imefikisha nguzo 520 za nishati ya umeme Mjini Babati Mkoani Manyara siku moja baada Rais John Magufuli kumuagiza Waziri wa Nishati Dk Merdad Kalemali kuhakikisha wananchi 4,000 waliolipia fedha za kuunganishiwa umeme wanapatiwa huduma hiyo.
Meneja wa shirika la ugavi wa nishati ya umeme (Tanesco) Mkoa wa Manyara, mhandisi Rehema Mashinji amesema nguzo hizo zimewasili Mjini Babati Octoba 26 saa nane mchana.
Mhandisi Mashinji ameipongeza kampuni ya kizalendo ya Qwihaya General ya Wilayani Mufindi Mkoani Iringa kwa kufikisha nguzo hizo kwa muda mfupi mara baada ya agizo la Rais Magufuli.
Amesema kampuni hiyo ilipopatiwa maelekezo na Serikali haikusubiri taratibu nyingine za kufanikisha suala hilo zaidi ya kubeba jukumu la kufikisha nguzo hizo mjini Babati.
“Namshukuru Rais Magufuli, Waziri wa Nishati Dk Kalemani na Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco kwa jitihada za dhati za kuchukua suala hili kwa uzito uliostahili na kuturahisishia kazi,” amesema mhandisi Mashinji.
Amesema Tanesco Mkoa wa Manyara imerahisishiwa kazi kwa nguzo hizo za awamu ya kwanza kufikishwa mjini Babati kwa lengo la kuhakikisha wananchi wa eneo hilo wanapatiwa huduma hiyo.
Amesema baada ya nguzo hizo kufikishwa mjini Babati mchakato wa kuwafungia umeme wananchi 4,000 waliolipia kila mmoja shilingi 27,000 utaanza mara moja.
Mkazi wa mtaa wa Dagailoi Mjini Babati, Mwanjaa Hamisi amepongeza hatua hiyo kwani ni muda mfupi tuu tangu Rais Magufuli alipomuagiza Waziri Kalemali kwenye uwanja wa Kwaraa na utekelezaji wake ukafanyika.
“Kutokana na kasi hii tuna uhakika baada ya siku chache tuu tutafanikisha kupatiwa umeme hivyo kusherehekea sikukuu ya Christmas tukiwa na umeme,” amesema.