Na John Walter-Babati
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Manyara, imetoa elimu ya kupambana na rushwa kwa wanafunzi wa Jeshi la Akiba ili waweze kupambana na kuepuka vishawishi vya rushwa wanapokuwa katika majukumu yao.
Mafunzo hayo yalitolewa Minjingu kata ya Nkaiti wilayani Babati na Ofisa wa TAKUKURU Dawati la Elimu mkoani humo .
Akizungumza na wanafunzi hao, Sultan Ng’aladzi alisema tatizo la rushwa limeenea kwenye jamii nzima hivyo ni jukumu la kila mtu kuhakikisha anakemea vitendo hivyo ambavyo hufanywa na kada mbalimbali.
“Vitendo hivi vinakwamisha jitihada za maendeleo kutokana na matumizi mabaya ya madaraka” alisema
Aliwataka wanafunzi hao wa Jeshi la Akiba kutoa taarifa katika ofisi za taasisi hiyo pindi wanapoombwa au kupiga namba ya bure 113 ili hatua staiki ziweze kuchukuliwa kwa wahusika.
“Kuna watu ambao wanajifanya wao ni Maofisa wa TAKUKURU mitaani ili kuwadanganya wananchi, nao mkiwaona toeni taarifa waweze kukamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria,” alisema.
Hata hivyo wanafunzi waliopatiwa mafunzo hayo wamesema awali hawakujua maana ya rushwa lakini kwa sasa baada ya mafunzo wapo tayari kutoa ushirikiano kwa Taasisi hiyo ili kukomesha vitendo hivyo ambavyo vinanyima wengine haki zao.