Baraza la madiani katika halmashauri ya mji wa Makambako limeutupia lawama wakala wa barabara za mijini na vijijini TARURA kwa kushindwa kutengeneza barabara kwa wakati hali ambayo imetajwa kuleta athari kubwa katika maendeleo ya uchumi.
Kutokana na hali mbaya ya miundombinu ya barabara wameiomba serikali kubadili kuzirejesha barabara hizo chini ya usimamizi wa baraza la madiwani kwa kuwa kumekuwa na uzembe mkubwa katika ukarabati huku pia wakidai kuwa hata chache zinazokarabatiwa zimekuwa hazi zingatii mahitaji ya watumia na umuhimu wake.
Mario Kihombo,Hanana Mfikwa ni baadhi ya madiwani ambao wamehoji uwezo mdogo wa kiutendaji wa TARURA ambao wamedai tangu kuingia kwake umeonekana kusuasua na kusababisha athari ya usafirishaji wa mazao na malighafi kutoka maeneo ya uzalishaji.
Licha ya kuonyesha kutorishwa na utendaji wa wakala huo lakini pia madiwani hao wameonyesha kukasirishwa na kitendo cha kuweka vibao vinavyozuia usafirishaji wa mizigo ya tani kumi katika barabara zilizochini yake hata zilizojengwa na wananchi kwamadai ya kwamba kufanya hivyo kunaua maghara,viwanda na masoko yailivyopo maeneo ya vijijini yanayohitaji magari makubwa kusafirisha bidhaa.
Mtandao huu umemtafuta meneja wa TARURA halmashauri ya mji wa Makambako mhandisi Boniventura Katambi ambaye anasema kinchokwamisha barabara nyingi kushindwa kukamilika kwa wakati ni kutokana na ufinyu wa bajeti ambapo kiasi cha shilingi mil 800 kikiwa kimetengwa na kueleza kwamba katika bajeti ya mwaka huu wakala huo umetoa kipaumbele katika ujenzi wa madaraja zaidi .
Serikali ya mkoa wa Njombe imetenga kiasi cha bil 8 katika mwaka wa fedha 2019/2020 za ujenzi wa miundombinu ya barabara za mijini na vijijini katika mkoa wa Njombe .