Mratibu wa mradi wa mijadala jumuishi katika masuala ya uchumi na utawala wa kifedha Alex Enock kutoka Shirika la Save The Children mkoani Shinyanga, akielezea madhumuni ya mradi na mafunzo.

Washiriki wakiwa kwenye mafunzo.
***************************************
Na Marco Maduhu -Shinyanga
Shirika la Save The Children ambalo linatetea haki za watoto, limetoa mafunzo ya mchakato wa bajeti ngazi ya halmashauri, ili kuisaidia Serikali uaandaaji wa bajeti nzuri ambayo itatoa dira ya maendeleo kwa kuzingatia vipaumbele vya wananchi.

Mafunzo hayo ambayo yatachukua siku mbili kuanzia leo, yameshirikisha watendaji wa Kata, wataalamu kutoka halmashauri ya manispaa ya Shinyanga, waandishi wa habari, pamoja na wadau kutoka mashirika mbalimbali yasiyo ya kiserikali,

Mratibu wa mradi wa mijadala jumuishi katika masuala ya uchumi na utawala wa kifedha, Alex Enock kutoka Shirika la Save The Children mkoani Shinyanga, alisema lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo wadau mbalimbali katika kushiriki kikamilifu kuandaa masuala ya bajeti, na kutambua wajibu wao katika kushiriki uundaji wa bajeti.

Amesema mradi huo wa masuala ya kibajeti utadumu ndani ya miaka miwili, ambapo ulianza june (2020) na utakoma Decemba (2021), ambao unatekelezwa Zanzibar maeneo ya unguja mjini, magharabi “A” na “B”, Mbozi mkoani Songwe, pamoja na manispaa ya Shinyanga, kwa ufadhili wa Ubalozi wa ulaya.

“Lengo pia la mafunzo haya ni kujenga uwezo kwa watendaji wa Serikali ngazi ya halmashauri, na wadau mbalimbali katika kupata elimu ya mchakato wa kibajeti ya Serikali, na kutambua miongozo inayo simamia michakato hiyo, ili kuisaidia Serikali katika utekelezaji wa haki za watoto hasa katika masuala ya kiafya, elimu, pamoja na kupinga matukio ya ukatili,” amesema Enock.
 

Naye Mgeni Rasmi akifungua mafunzo hayo Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu Mkoa wa Shinyanga, Joachim Otaru, amewataka washiriki hao wayashike vizuri mafunzo hayo, na kwenda kuyafanyia kazi kwa vitendo katika uaandaji wa bajeti, kwa kuzingatia vipaumbele vya wananchi pamoja na kushirikisha makundi yote.
 
“Mafunzo haya ya bajeti ni muhimu sana, sababu yanagusa maisha yetu, hivyo na waomba katika uaandaji wa bajeti ijayo ya Serikali, mshirikishe wadau na makundi yote kuanzia ngazi ya chini,”amesema Otaru.

Kwa upande wake mwezeshaji wa mafunzo hayo ya kibajeti mchumi kutoka ofisi ya mkuu wa mkoa wa Shinyanga Allex Mpasa, amesema kuwa sasa hivi bajeti hua zinaandaliwa kwa kuzingatia jitihada za wananchi, na siyo kuzingatia vipaumbele vyao, jambo ambalo siyo sahihi.

Nao baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo hasa watendaji wa Serikali, walishukuru kupewa elimu hiyo ambayo itakuwa msaada mkubwa kwao, katika uaandaji wa bajeti kwa kuzingatia vipaumbele vya wananchi, na kuacha kufanya kazi kwa mazoea.