WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amefanya ziara ya kushtukiza leo Jumapili, Agosti 23, 2026, katika Hospitali ya rufaa ya Mkoa Mwananyamala, jijini Dar es Salaam, kukagua hali ya utoaji wa huduma kwa wananchi.

Alipowasili hospitalini hapo, Dkt. Mwigulu ametembelea wodi mbalimbali, zikiwemo Wodi ya Mama na Mtoto na Wodi ya Upasuaji, ambako amezungumza na wagonjwa pamoja na ndugu zao na kusikiliza maoni yao kuhusu huduma zinazotolewa hospitalini hapo na changamoto wanazokabiliana nazo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wananchi wanaopata huduma hospitalini hapo wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Serikali kwa ujumla kwa kuendelea kuboresha huduma za afya na mazingira ya utoaji wa huduma hospitalini hapo.

Katika ziara hiyo, Waziri Mkuu aliambatana na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila; Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Saad Mtambule; pamoja na viongozi wa Hospitali hiyo.