Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia), akiteta na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Beno Malisa, wakati akiwasili katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, baada ya kufika mkoani humo kwa ajili ya kuhitimisha sherehe za Maadhimisho ya Nane-Nane yaliyofanyika katika viwanja vya John Mwakangale.

Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia), akisaini Kitabu cha wageni alipofika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, baada ya kufika mkoani humo kwa ajili ya kuhitimisha sherehe za Maadhimisho ya Nane-Nane yaliyofanyika katika viwanja vya John Mwakangale. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Mbeya)

…………

Na. Joseph Mahumi, WF, Mbeya

Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuimarisha sekta ya miundombinu nchini ili iweze kuchochea ukuaji wa uchumi, hususan katika sekta za uzalishaji kama kilimo cha chai na mazao mengine yanayozalishwa katika Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati alipofika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, kwa ajili ya kuhitimisha sherehe za Maadhimisho ya Nane-Nane yaliyofanyika katika viwanja vya John Mwakangale, jijini Mbeya jana.

Mhe. Balozi Omar alisema, Serikali imejipanga kuhakikisha upatikanaji wa fedha za miradi ya miundombinu unakuwa wa uhakika, ili kuwezesha utekelezaji wa miradi hiyo kwa wakati na kwa ufanisi.

Alisema kuwa changamoto ya muda mrefu imekuwa ni ucheleweshaji wa fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo, jambo lililosababisha kusuasua kwa utekelezaji wa miradi mingi ya barabara na miundombinu mingine muhimu kwa uchumi. Hata hivyo, alieleza kuwa Serikali imefanya mageuzi ya kimfumo kwa kuamua kwamba asilimia 70 ya mapato yanayokusanywa kupitia mifuko maalum yataelekezwa moja kwa moja kwenye mifuko hiyo bila kupita Hazina.

“katika mwezi wa Julai pekee, jumla ya shilingi bilioni 324 zilitolewa kwa mifuko mbalimbali ya maendeleo, ambapo shilingi bilioni 76 zilipelekwa moja kwa moja kwenye Mfuko wa Barabara na utaratibu huu utaendelea kwa mwaka mzima wa fedha ili kuhakikisha miradi ya miundombinu haikwamishwi na uhaba wa fedha” alisema Mhe. Balozi Omar.

Aliongeza kuwa pamoja na utaratibu huo, Serikali inashirikiana na sekta ya fedha kutafuta njia mbadala za kupata fedha nyingi mapema kupitia mifumo kama hati fungani za miundombinu (infrastructure bonds), ili kuwezesha utekelezaji wa miradi mikubwa kwa wakati badala ya kusubiri mapato ya ndani kukusanywa kidogo kidogo.

Aidha, Mhe. Balozi Omar alisema kuwa umuhimu wa miundombinu hasa barabara, ni kiungo muhimu cha kiuchumi kinachowawezesha wakulima kufikisha mazao yao sokoni kwa urahisi na kwa gharama nafuu.

“Maeneo haya ya Nyanda za Juu Kusini, ambako zao la chai na mazao mengine ya kilimo huzalishwa kwa wingi, miundombinu bora ya barabara itasaidia kuongeza tija kwa wakulima na kuchochea ukuaji wa viwanda vya kuongeza thamani ya mazao hayo lakini pia tunarahisisha usafirishaji wa mazao, tunapunguza upotevu wa bidhaa, na tunafungua fursa za masoko mapya. Hii ndiyo njia ya kuongeza kipato cha wakulima na kukuza uchumi wa nchi,” alisema  Mhe. Balozi Omar

Mhe. Balozi Omar aliongeza kuwa Serikali itaongeza usimamizi katika utekelezaji wa miradi ili kuhakikisha wakandarasi wanazingatia mikataba yao na kuonya kuwa wakandarasi watakaobainika kuchelewesha miradi bila sababu za msingi watachukuliwa hatua kali, ikiwemo kuwekwa kwenye orodha ya kutopatiwa kazi nyingine za Serikali kwa suala la miundombinu si ajenda ya kisiasa bali kama suluhisho la changamoto za wananchi, kwa kuwa hali mbaya ya barabara katika baadhi ya maeneo imekuwa kikwazo kwa shughuli za kiuchumi, hususan katika sekta za uzalishaji.

Kwa Upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Beno Malisa, alieleza kuwa Mkoa huo unatambua na kuthamini jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali katika kuboresha miundombinu, hususan baada ya kutolewa kwa zaidi ya shilingi bilioni 9 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya njia nne (Igawa-Uyole-Songwe-Tunduma), ambapo hatua hiyo ni ya kihistoria kwa Mkoa huo kwani itarahisisha usafiri na usafirishaji wa bidhaa, kupunguza msongamano wa magari, na kufungua fursa mpya za kiuchumi kwa wananchi na wawekezaji.

“Pamoja na maboresho ya barabara, Serikali imeendelea kuwekeza katika huduma muhimu kama umeme na maji, ambapo TANESCO tayari imetoa ratiba ya kupeleka umeme katika maeneo yaliyokuwa na uhitaji mkubwa” alisema Mhe. Malisa

Alibainisha kuwa uwepo wa umeme katika maeneo ya uzalishaji, ikiwemo migodi inayozalisha hadi kilo 400 za dhahabu kwa mwezi, utaongeza tija na thamani ya uzalishaji huo, lakini pia alisisitiza kuwa maboresho ya huduma za maji na miundombinu mingine yataendelea kuimarisha ustawi wa wananchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Mbeya.