Na Mwandishi Wetu
Julai 25, 2026, dunia itaadhimisha miaka mitano tangu kuanzishwa kwa Siku ya Kimataifa ya Kuzuia Vifo vya Kuzama Maji Duniani, ikiwa ni wito wa kuimarisha hatua za pamoja dhidi ya moja ya visababishi vya vifo vinavyoweza kuzuilika kwa urahisi.
Kwa mujibu wa ujumbe wa kimataifa wa mwaka 2026, tangu mwaka 2000 kiwango cha vifo vinavyotokana na kuzama maji duniani kimepungua kwa asilimia 38, jambo linaloonyesha kuwa hatua za kinga zina matokeo chanya. Hata hivyo, zaidi ya watu 300,000 bado hufariki kila mwaka kutokana na kuzama maji, huku wastani wa watu 30 wakipoteza maisha kila saa.
Takwimu zinaonyesha kuwa asilimia 92 ya vifo hivyo hutokea katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati. Watoto ndio wanaoathirika zaidi, ambapo asilimia 24 ya vifo vyote vya kuzama maji ni watoto wenye umri chini ya miaka mitano. Aidha, kuzama maji ni sababu ya tatu kwa ukubwa ya vifo kwa watoto wenye umri wa miaka 5 hadi 14, na sababu ya nne kwa watoto wa miaka 1 hadi 4.
Ujumbe huo pia unaeleza kuwa asilimia 75 ya vifo vinavyotokea wakati wa mafuriko husababishwa na kuzama maji. Wataalamu wanaeleza kuwa kuwekeza katika hatua muhimu za kinga, ikiwemo kuwafundisha watoto kuogelea na kuboresha usalama wa maeneo yenye maji, kunaweza kuokoa maisha ya watu zaidi ya 774,000 ifikapo mwaka 2050, huku kila fedha inayowekezwa ikitarajiwa kurejesha faida mara tisa.
Kaulimbiu ya mwaka huu inasisitiza kuwa kila mtu ana nafasi ya kushiriki katika kuzuia vifo vya kuzama maji. Wazazi na walezi wanahimizwa kuwafuatilia watoto kwa karibu wanapokuwa karibu na maji, kufunika au kuzungushia uzio visima, matenki na vyombo vya kuhifadhi maji, pamoja na kuwafundisha watoto ujuzi wa kuogelea na usalama majini. Pia wanashauriwa kujifunza huduma ya kwanza ya uokoaji (CPR).
Jamii nayo inahimizwa kushirikiana kulinda watoto, kutoa elimu ya usalama majini, kuripoti mazingira hatarishi na kuandaa mafunzo ya kuogelea na uokoaji. Viongozi wa jamii wanatakiwa kubaini na kuondoa maeneo hatarishi, kuimarisha mifumo ya tahadhari ya mafuriko, kuhakikisha usalama wa watu wanaofanya kazi au kusafiri majini, pamoja na kuhamasisha sera zinazolinda maisha ya wananchi.
Ujumbe wa kimataifa wa mwaka 2026 unahitimisha kwa kusisitiza kuwa kuzuia kuzama maji si jukumu la serikali pekee, bali ni wajibu wa kila mmoja nyumbani, shuleni, sehemu za kazi na katika jamii, ili kuokoa maisha na kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika.
