Na. Fullshangwe Blog, Bungeni Dodoma
Serikali imesema uchumi wa Tanzania umeendelea kuimarika kutokana na utekelezaji wa sera madhubuti za kiuchumi, uwekezaji katika miradi ya maendeleo na kuendelea kuimarika kwa mazingira ya biashara nchini.
Akiwasilisha Mapendekezo ya Mpango na Bajeti ya Wizara ya Fedha kwa mwaka 2026/27 bungeni jijini Dodoma, Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar amesema kuwa uchumi wa Taifa umeendelea kuhimili changamoto mbalimbali za kiuchumi zilizojitokeza katika ngazi ya dunia.
Amesema kuwa ukuaji wa uchumi umechochewa na kuimarika kwa shughuli za uzalishaji katika sekta mbalimbali pamoja na uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika miundombinu ya kimkakati.
Aidha, amebainisha kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji kwa kuondoa vikwazo vya kibiashara, kurahisisha huduma kwa wawekezaji na kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi.
Pia ameongeza kuwa hatua hizo zimechangia kuongezeka kwa mtaji wa uwekezaji, uzalishaji wa bidhaa na huduma pamoja na fursa za ajira kwa wananchi.
Amebainisha Kuwa Serikali itaendelea kutekeleza sera zinazolenga kukuza uchumi shindani, kuongeza ushiriki wa sekta binafsi na kuvutia uwekezaji wa ndani na nje ya nchi.
Ameeleza kuwa mwenendo mzuri wa uchumi unaendelea kuweka msingi imara wa kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa na kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.
