Na. Meleka Kulwa-Fullshangwe Blog, Dodoma
WATUMISHI wa umma wanaojihusisha na kughushi barua za uhamisho na nyaraka nyingine za kiutumishi wameonywa kuacha mara moja tabia hiyo, huku Serikali ikieleza kuwa tayari watuhumiwa sita wamefikishwa mahakamani kwa makosa ya uhujumu uchumi yanayohusiana na vitendo hivyo.
Onyo hilo limetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, Juni 1,2026 wakati akifungua kikao kazi cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu jijini Dodoma.
Waziri Kikwete amesema baadhi ya watumishi wamekuwa wakighushi barua za uhamisho ili kuhamia maeneo ya mijini au sehemu zenye maslahi makubwa, jambo ambalo ni kinyume cha sheria, kanuni na maadili ya utumishi wa umma.
Amesema Ofisi ya Rais-UTUMISHI kwa kushirikiana na taasisi za haki jinai imeanza kuwachukulia hatua wahusika, ambapo hadi sasa watuhumiwa sita wamefikishwa mahakamani huku wengine wakitarajiwa kufikishwa kwenye vyombo vya sheria baada ya uchunguzi kukamilika.
Aidha, amewataka waajiri kuchukua hatua za kinidhamu dhidi ya watumishi wote watakaobainika kuhusika na kughushi nyaraka za kiutumishi na kuhakikisha taarifa za utekelezaji zinawasilishwa kwa wakati.
