Na Prisca Libaga RAS Arusha
Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro ameeleza kufurahishwa na mwitikio mkubwa wa watu wanaojitokeza kupata msaada wa kisheria kwenye Kampeni ya Mama Samia Jijini Arusha, akisema kampeni hiyo si tu ya Watanzania bali ni ya kila mmoja anayeishi nchini kama ambavyo leo Machi 04, 2025 aliposikiliza na kutatua mgogoro wa zaidi ya miaka saba uliowahusisha raia kutoka nchini Italia.
Waziri Ndumbaro ambaye yupo Mkoani hapa kukagua na kushiriki katika utoaji wa huduma hiyo, ikiambatana na shamrashamra za wiki ya wanawake, amesema Wizara yake imebaini pia mambo kadhaa ikiwemo kiu ya wananchi kupata elimu ya sheria pamoja na uelewa mdogo wa njia za utatuzi wa migogoro kwa wananchi.
Wakizungumza mara baada ya kumalizika kwa shauri lao, Raia hao wa Italia ambao waliungana watatu na kuanzisha Kampuni na baadae kutokea kutokuelewana miongoni mwao, wameishukuru Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa msaada huo, wakikiri kuwa ndani ya saa moja, wamefanikiwa kuumaliza mgogoro uliodumu kwa miaka zaidi ya saba, wakitishiana kuchomana visu na kudhuriana kwenye biashara zao.




