Mafundi wakiendelea na ujenzi wa daraja linalounganisha Kijiji cha Bukokwa na Sukuma,katika Halmashauri ya Buchosa, Sengerema .Daraja hilo linajengwa kwa michango ya vijana na watoto waliozaliwa na kusoma katika kijiji hicho ambao kwa sasa wanaishi na kufanya kazi kwenye mikoa mbalimbali nchini.Picha na Baltazar Mashaka
Mwenyekiti wa Kijiji cha Sukuma, Edwin Sagini Tibezuka,akimwonyesha mwandishi wa Uhuru Vijijini (hayupo pichani) miundombinu ya daraja la barabara ya Sukuma -Kalebezo ilivyoharibika na kutopitika.Picha na Baltazar Mashaka
Mwenyekiti wa Kijiji cha Sukuma, Edwin Sagini Tibezuka, akipita kulia mwa daraja lingine la moja ya barabara linalounganisha kijiji hicho na Nyashana juzi.Picha na Baltazar Mashaka 

 …………………………………………………

NA BALTAZAR MASHAKA, Buchosa
 
VIJANA wazawa wa Kijiji cha Sukuma,Halmashauri ya Buchosa, wilayani Sengerema,wanaoishi na kufanya kazi maeneo mbalimbali nchini wamehamasishana na kuchangia fedha na vifaa vya kujenga daraja la kudumu linalounganisha kijiji hicho na Kijiji cha Bukokwa.

Daraja hilo kwa muda mrefu lilikuwa halipitiki na kusababisha mawasiliano ya barabara kukatika ambapo wakati wa masika iliwawia vigumu wananchi kuvuka ng’ambo ya pili kupata huduma ya usafiri wa magari kwenye barabara kuu ya Sengerema-Bukokwa-Nyehunge ya urefu wa km 53.

Wakizunguma na Uhuru Vijijini baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Sukuma na Mwamanyili, wapongeza vijana wazawa kujenga daraja hilo na kuwaondolea kero na changamoto ya muda mrefu ya kukosa daraja la kudumu.

“Nawapongeza vijana wetu kwa kuona mbali zaidi na kujenga daraja, haijawahi kutokea tangu kuanzishwa kwa kijiji hiki mwaka 1974,wameielewa vizuri kauli ya Rais Samia Suluhu Hassan ya Kazi Iendelee,”alisema mmoja wa wazazi wa vijana waliohamasika kujenga daraja hilo huku akiomba hifadhi ya jina kwa hofu za kisiasa.
 
Naye Masalu Segeja mkazi wa Kijiji cha Mwanyamili,alisema kitendo cha kujenga daraja kilichofanywa na ndugu zao ili kuwasaidia wazazi ni cha kupongezwa na kulaani anayetaka kukwamisha kuwa wanahujumu miundombinu ya daraja

Mmoja wa vijana hao waliozaliwa na kusoma kwenye Kijiji cha Sukuma (jina linahifadhiwa) akizungumza kwa niaba ya wenzake, alisema kila wanapofunga safari kuja kijiji wakiwa na magari wanalazimika kuyaacha Kijiji cha Bukokwa baada ya daraja kuharibika kwa miaka 47.

Alisema daraja la zamalini lilivunjika na kumezwa na maji,hivyo kusababisha baadhi ya watoto kusombwa na maji wakati wa mvua za masika, hasa wanafunzi waliokuwa wakisoma shule ya sekondari Nyakarilo, licha ya diwani aliyepita kulifanyia ukarabati bado lilionekana kuhatarisha maisha ya watu.

Alieleza kuna changamoto kwenye vijiji vya pembezoni vya Nyabutanga, Mwamanyili, Sukuma na Bukokwa kutokana na kuzungukwa na mito na majaruba ya mpunga,ukifika Bukokwa ukiwa na gari unalazimika kuliacha ili uvuke mto kwa miguu kwenda nyumbani.

“Tangu enzi hatujawahi kuwa na miundombinu bora na imara ya barabara na madarajaya uhakika baada ya yaliyojengwa zamani kuvunjika,vijana tupo wengi Dar es Saalam,Mwanza, Mtwara na kwingineko,kwa wingi huo tunaweza kufanya kitu,hivyo kwa uwezo wetu tukachanga fedha za kujenga daraja tukapata zaidi y ash. milioni 10,”alisema.

Hata hivyo, alidai baada ya upembuzi yakinifu wa ujenzi wa daraja hilo,yaliibuka wanafanya hivyo kwa maslahi ya kisiasa  na kusistiza wao hawana itikadi kisiasa wanachotaka ni maendeleo ya wananchi,kwani miongoni mwao wamo viongozi serikalini ambao hawataki kujiingiza ama kuingizwa kwenye siasa n wanaishukuru TARURA kwa kuwaunga mkono na kubariki mradi huo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kijiji cha Sukuma,Edwin Sagini Tibezuka, aliwashukuru vijana wanaoishi nje ya kijiji hicho kwa kuamua kujenga daraja ambalo limekuwa kero na kuhatarisha maisha ya wananchi.

Pia alisema serikali imewasahau kwenye ujenzi wa barabara, madaraja na huduma ya maji safi kwa matumizi ya jamii ambapo zaidi ya kaya 620 za vitongoji vitano,zinategemea kisima kimoja cha asili na wakati wa kiangazi ni changamoto.

Alisema barabara zinazounganisha kijiji hicho na vijiji jirani ni mbovu na wakati wa mvua hazipitiki na kuzitaja kuwa ni Bukokwa-Magata (km 7) kuelekea mpakani mwa Geita,Lubanja- Luchili-Sengerema,Mwamanyili-sukuma (km 5), Sukuma-Kalebezo daraja limekatika pia Sukuma-Nyashana haipitiki.

Aidha ibezuka alikanusha madai kuwa kiongozi mmoja anakwamisha maendeleo ukiwemo ujenzi wa daraja,licha ya kukiri kusikia uvumi wa tuhuma hizo, kama angezuia ujenzi usingeendelea, na hata wananchi wamejitolea kuunga mkono jitihada za watoto wao kwa kuchangia (mawe,mchanga na maji) ambapo uongozi wa kijiji ulishirikishwa.