Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Dodoma, Sosthenes Kibwengo,akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani)

………………….

Na Alex Sonna,Dodoma

TAASISI ya kuzuia na kupambana na rushwa nchini (TAKUKURU) mkoa wa Dodoma, imewataka wanawake kutoa taarifa dhidi ya vitendo vya rushwa ya ngono vinavyofanywa makazini dhidi yao ili kuisaidia taasisi hiyo kutokomeza ukatili huo unavyofanywa kwa kificho.

Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Dodoma, Sosthenes Kibwengo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na rushwa ya ngono inayoendelea katika sekta mbalimbali hapa nchini.

Kibwengo alisema tatizo hilo lipo katika sekta binafsi, taasisi za
umma hata majumbani, lakini taarifa haziwafikii TAKUKURU kiufasaha kutokana na walengwa kuhofia kuzitoa kwa kuogopa watajulikana.

“Tunaomba wanawake muwe na ujasiri wa kutoa taarifa juu ya vitendo hivyo, kwa sababu hakuna sheria inayoruhusu mtu kunyanyaswa kijinsia kazini TAKUKURU itakulinda” alisema Kibwengo.

Kibwengo alisema kumekuwa na matukio mengi ya aina hiyo kwenye jamii lakini taarifa ya tuhuma zilizowasilishwa ni chache kulingana na uhalisia wa jambo lenyewe ndio maana wameamua kutoa taarifa hiyo na kuitaka jamii kutoa ushirikiano ili kutokomeza unyanyasaji wa aina hiyo.

“Tumeletewa tuhuma chache kipindi hiki haziendani na hali halisi
ilivyo mitaani hususani katika sehemu za kazi” alisema Kibwengo.

Alifafanua kuwa hivi sasa Taasisi hiyo imeanzisha Dawati
maalumu la jinsia la kushughulikia vitendo vya unyanyasaji wa kingono kwa wanawake na wanaume kama wapo wanaofanyiwa vitendo hivyo.

“Naomba jamii isisite kutoa taarifa kama wanafanyiwa vitendo hivyo kwasababu ni kinyume na sheria namba 25 ya mwaka 2007 ambayo inakataza suala la ngono kazini ”alisema Kibwengo.

Kutokana na hili alisema hakuna sababu ya jamii kuogopa kutoa taarifa ya kuwa ananyanyaswa kijinsia iwe kazini au nyumbani,kinachotakiwa ni kutoa taarifa yenye ukweli ndani yake na wao watachukua hatua ya kuchunguza na kubaini kama inaukweli na baadae watachukua hatua stahiki za kisheria.

Alisema lengo lao ni kuona rushwa inatokomezwa katika sehemu za kazi hususani kwa wanawake ambao wamekuwa wakinyanyaswa kijinsia katika maeneo ya kazi wanayofanyiwa jambo ambalo halileti picha nzuri kwa jamii kwa ujumla.

“Hata kama kuna wanaume wananyanyasika kingono kazini kupitia
mwanamke naye anapaswa kutoa taarifa kwa sababu hakuna sheria inayoruhusu mtu kunyanyaswa kijinsia akiwa kazini” alisema Kibwengo.

Kutokana na hilo taasisi hiyo imeiomba jamii kutoa taarifa pale
wanapoona wananyanyaswa kijinsia ili kuisaidia taasisi hiyo iweze
kubaini na kukomesha watu wanaotumia madaraka vibaya kwa ajili ya kuwanyanyasa wengine.

“Wote wanaotumia nafasi zao za madaraka kuomba rushwa ya ngono ni kinyume na sheria kwani endapo watabainika nao watawajibishwa ikiwemo kupelekwa mahakamani”alisema Kibwengo.

Alisema watu wamekuwa wakijificha hawako huru kutoa taarifa ya vitendo hivyo hata kama kunadalili za rushwa ya ngono au wametoa rushwa ya ngono jambo ambalo sio sahihi kabisa.

Kutokana na hilo ameiomba jamii kuwa wazi kwa taasisi hiyo,kwa sababu iko kwa ajili ya kuisaidia jamii na sio kuiangamiza.

Akizungumzia suala la utapeli unaofanywa na baadhi ya watu wakijifanya ni maafisa TAKUKURU na kuwatishia wananchi alisema wananchi wanapaswa kuwa makini na watu wa aina hiyo kwa sababu taasisi hiyo haitoi vitisho kwa jamii bali inafanya kazi kwa ushirikiano na wananchi.