Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Umma, Jaji Mstaafu Hamisa Kalombola, amewataka watumishi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, uadilifu, uzalendo na uwajibikaji katika kutekeleza majukumu yao kwa maslahi ya taifa.
Jaji Mstaafu Hamisa Kalombola alitoa kauli hiyo wakati wa kikao na watumishi wa NCAA, ambapo Tume hiyo ilikutana na watumishi kwa ajili ya kukumbushana kuhusu haki, wajibu, maadili na misingi ya utumishi wa umma.
Akiwa ameambatana na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma, Bw. Nolasco Kipanda, pamoja na viongozi na watendaji wengine wa Tume hiyo, Jaji Mstaafu Kalombola alisisitiza kuwa utumishi wa umma ni dhamana inayohitaji kila mtumishi kutekeleza wajibu wake kwa uaminifu, weledi na kuzingatia maslahi mapana ya taifa.
“Kila mmoja ana wajibu wa kutekeleza kwa mwenzake ili kujenga utumishi wa umma wenye ufanisi na unaoaminika,” alisema Jaji Mstaafu Hamisa Kalombola.
Alisisitiza pia umuhimu wa watumishi kutunza siri za Serikali, kufanya kazi kwa uzalendo na kuzingatia uadilifu.
Kwa upande wake, Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma, Bw. Nolasco Kipanda, alisema Tume inaendelea kutekeleza jukumu lake la kufanya ukaguzi katika taasisi na mashirika ya umma kwa lengo la kuhakikisha sheria, kanuni, taratibu na misingi ya utumishi wa umma inazingatiwa.
Akizungumza katika kikao hicho naibu kamishna wa Uhifadhi wa NCAA Joas Makwati amesema mamlaka itafanyia kazi maelekezo ya Tume hiyo ili kihakikisha hakuna hoja za ukaguzi katika masuala ya utumishi na maeneo mengine

