Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amempongeza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, kwa uteuzi wake katika wadhifa huo na kumtaka kuendelea kufanya kazi kwa bidii katika kutekeleza majukumu yake.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 19 Agosti 2026, alipokutana na Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, aliyefika Ikulu Zanzibar kujitambulisha rasmi kufuatia uteuzi wake kuwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, pamoja na kupokea maelekezo kuhusu utekelezaji wa majukumu yake mapya.

Rais Dkt. Mwinyi amesema ana imani na uwezo wa Ndg. Abdi katika wadhifa huo, kutokana na uzoefu na utendaji aliouonesha alipokuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Zanzibar.

Rais Dkt. Mwinyi ameeleza kuwa wadhifa huo una wigo mpana wa majukumu yanayohusu masuala mbalimbali ya kisiasa, kiuchumi na kijamii, hivyo unahitaji juhudi, umakini na ushirikiano wa karibu na viongozi pamoja na watendaji wengine wa Chama ili kuhakikisha majukumu hayo yanasimamiwa na kutekelezwa kwa ufanisi.

Rais Dkt. Mwinyi amemtakia Ndg. Abdi mafanikio katika wadhifa wake mpya na kumhimiza kuendelea kufanya kazi kwa bidii.

Naye, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, amemshukuru Rais Dkt. Mwinyi kwa maelekezo na ushauri aliompatia, pamoja na imani aliyooneshwa katika uteuzi wake.

Ndg. Abdi ameahidi kufanya kazi kwa bidii na kushirikiana na viongozi na watendaji wenzake katika kutekeleza majukumu ya wadhifa huo na majukumu mengine atakayokabidhiwa na Chama.