Katika jitihada za kukuza ushirikiano kati ya taasisi za mafunzo na wenye viwanda na waajiri, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Hussein Mohamed Omar amehimiza Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kuingia makubaliano na kampuni ya Hans Paul ya jijini Arusha inayojihusisha na kutengeneza na kubadili bodi za magari ya utalii (Safari vehicles).
Akizungumza wakati wa ziara yake katika kampuni hiyo leo, tarehe 19 Agasti, 2026 Dkt. Omar amesema ipo haja ya VETA kuwa na makubaliano rasmi na kampuni hiyo ili kuleta mageuzi katika utoaji mafunzo ya ufundi wa magari ya kisasa amabayo yanahitajika sana katika sekta ya utalii
“Kwa kuingia makubaliano hayo vijana wetu kutoka vyuo vya VETA watapata fursa ya kujifunza mambo mengi kwa vitendo katika sekta hii ya ufundi wa magari, hususan magari yanayotumika katika shughuhuli za utalii hapa nchini,” amesema Dkt. Omar.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, VETA, Dkt. Abdallah Ngodu akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa VETA amsema itatumia fursa ya ushirikiano huo kama sehemu muhimu ya utekelezaji wa mtaala mpya wa ufundi magari.
“VETA tumeandaa mtaala wa ufundi wa magari, hususan magari yanayotumia umeme. Baada ya kutembelea hapa tumeona wanatengeneza magari yanayotumia umeme na mengine yanatumika katika huduma za utalii,” amesema.
Aidha Dkt Ngodu amebainisha Kuwa baada ya ziara katika kampuni hiyo wamegundua ipo haja ya kuaandaa mtaala unaohusu madereva wanaondesha magari ya utalii na wenye ujuzi wa kuwaongoza.
“Ziara hii imekuwa na tija, kwani mmiliki wa kampuni hii amekubali vijana wetu kuendelea kupata mafunzo ya vitendo hapa pamoja na wakufunzi kuja kupata ujuzi zaidi ili waweze kutoa mafunzo yatakayowawezesha vijana kuendana na uhitaji wa soko la ajira,” ameongeza Dkt. Ngodu.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Hans Paul, Satbir Singh Hanspaul amesema wataendelea kushirikiana na VETA pamoja vyuo vingine vinavyotoa mafunzo ya ufundi, hususan wa magari kwa lengo la kuendelea kuwapa vijana ujuzi wa vitendo.
Hata hivyo ameziomba kampuni nyigine binafsi kuendeleza ushirikiano na taasisi za seriakli ilikupata matokeo chanya hapo baadae.
Satbir Singh amehitimisha kwa kiushukuru serikali ya awamu ya sita pamoja Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kuona umuhimu wa kuishirikisha sekta binafsi ili kuleta matokeo chanya katika sekta ya elimu.

