ASISITIZA DHAMIRA YA SERIKALI YA KUJENGA UCHUMI SHINDANI WA VIWANDA ILI KUFIKISHA NCHI UCHUMI WA KIPATO CHA KATI CHA JUU

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imedhamiria kujenga uchumi shindani wa viwanda ili kuifikisha nchi kwenye kipato cha kati cha juu.

 

Makamu wa Rais amesema hayo wakati wa hafla ya utoaji wa tuzo za Jubilei ya Dhahabu ya Maadhimisho ya Miaka 50 ya Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) iliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam. Amesema katika kufikia azma hiyo, Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji kwa kiwango kikubwa, utungaji wa sera sahihi, ujenzi wa miundombinu, uimarishaji wa Taasisi na kuwezesha sekta binafsi kufanya biashara kwa ufanisi zaidi.

Makamu wa Rais amesema, katika kipindi cha miaka 50 iliyopita, Maonesho ya Sabasaba yamejenga msingi wa ushindani kibiashara, yamechochea ukuaji wa biashara na kujenga uwezo wa wafanyabiashara na wazalishaji, na kuimarisha uhusiano baina ya wazalishaji na walaji.

Amesema katika safari ya kuelekea mwaka 2050, maonesho hayo yanapaswa kuwa miongoni mwa maonesho makubwa zaidi ya biashara duniani, yakiiweka Tanzania kama kitovu cha biashara, uwekezaji, ubunifu na viwanda barani Afrika.

Halikadhalika, Makamu wa Rais ametoa wito kwa wazalishaji wote nchini kuitumia ipasavyo alama maalum ya bidhaa za Tanzania, yaani Made in Tanzania iliyoanzishwa hivi karibuni ili kujenga hadhi ya bidhaa za Tanzania na kuongeza ushindani wake katika masoko ya Afrika na duniani.

Makamu wa Rais amesema ili kutoa mchango stahiki katika utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050, ni vema kufanya mabadiliko makubwa zaidi katika sekta ya viwanda na biashara, ikiwemo uzalishaji wa bidhaa zenye thamani kubwa, na kutumia teknolojia za kisasa katika uzalishaji. Amesema ni muhimu kuongeza ubunifu ili kuanzisha kampuni zitakazozalisha bidhaa zenye ubora na ushindani katika masoko.

Aidha, amesema masuala ya utafiti, ubunifu na matumizi ya akili unde, biashara za kidijitali na mifumo ya kisasa ni lazima viwe sehemu ya ukuaji wa uchumi.

Vilevile, Makamu wa Rais ametoa rai kwa Taasisi za fedha kujielekeza zaidi kusaidia katika kutoa mitaji kwa sekta ya viwanda, hususan viwanda vidogo vidogo kwa kuweka masharti ya mikopo ya upendeleo kwa viwanda vidogo na vya kati. Amezipongeza Taasisi za fedha ambazo tayari zinatoa huduma hiyo hatua inayosaidia kupunguza vikwazo vinavyosababisha wajasiriamali wengi kushindwa kupata mikopo.  

Kwa upande wake, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga amesema mafanikio yaliyopatika katika kipindi cha miaka 50 ya maonesho ya Sabasaba yametokana na ushirikiano wa pamoja kati Serikali na Sekta Binafsi, ikiwemo wafanyabiashara waliothubutu kuwekeza mitaji yao, kuzalisha bidhaa, kukidhi viwango na kuingia katika masoko mapya.

 

Mhe. Kapinga amewashukuru wakulima, wazalishaji wa bidhaa, wafanyabiashara, wauzaji wa bidhaa, washirika wa maendeleo, wabunifu na Taasisi mbalimbali, kampuni na wawekezaji waliofanya kazi na TanTrade katika kipindi cha miaka 50 ya maonesho hayo.

 

Awali akitoa maelezo ya hafla ya tuzo hizo, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade), Dkt. Latifa Khamis amesema katika kipindi cha Miaka 50 jukwaa hilo limezalisha fursa ya thamani ya shilingi Trillion129.2 ikichochea ukuaji wa uchumi na kuimarisha nafasi ya Tanzania katika ramani ya biashara ya kimataifa.