Tanzania inashiriki katika Mkutano wa Wataalam wa Kamati ya Mawaziri wa Sheria na Wanasheria Wakuu wa Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), unaofanyika Victoria Falls nchini Zimbabwe, kuanzia tarehe 1 hadi 4 Juni, 2026.
Mkutano huo ni sehemu ya maandalizi ya Mkutano wa Kamati ya Mawaziri wa Sheria na Wanasheria Wakuu wa Serikali wa SADC utakaofanyika tarehe 5 Juni, 2026.
Lengo la Mkutano huo, ni kujadili masuala mbalimbali ya Kisekta na kupitia nyaraka za Sheria za Jumuiya ambazo zitawasilishwa na kujadiliwa na Mawaziri na Wanasheria Wakuu wa Serikali.
Pamoja na mambo mengine, Mkutano huo umejadili namna sekta ya sheria inaweza kusaidia malengo ya Jumuiya ikiwemo kuhakikisha Itifaki na Nyaraka za sheria za SADC zinasainiwa na kuridhiwa kwa wakati.
Aidha, Mkutano huo umeweka mikakati itakayosaidia nchi wanachama kuwasilisha changamoto zilizopo katika Itifaki na Nyaraka zingine za sheria za SADC ili kuhakikisha nyaraka zote za sheria zinapitishwa bila kuathiri Katiba, miongozo na sheria za nchi wanachama.
Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huo unaongozwa na Bi. Felista Lelo, Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Mikataba kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, akiambatana na Bi. Angella Kimaro Kaimu Mkurugenzi Idara ya Uratibu na Masuala ya Sheria kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Abdulrahman Mshamu Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Sheria kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, na Bi. Shazma Msuya kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

