Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti (katikati) akiwa na Katibu Tawala Mkoa huo Denis Bandisa (kulia) na Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga Sebastian Waryuba (kushoto) wakati wa kikao cha kamati ya Afya ya Msingi Mkoa kuhamasisha viongozi juu kwenda kuhamasisha wananchi wajitokeze kupata chanjo dhidi ya UVIKO-19.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti akifungua kikao cha kamati ya Afya ya Msingi Mkoa kuhusu utekelezaji wa Mpango Harakishi wa utoaji chanjo dhidi ya UVIKO-19 juzi mjini Sumbawanga.
Kiongozi wa Machifu Mkoa wa Rukwa Charles Katata Milanzi toka Nkasi akichangia kuhusu umuhimu wa chanjo ya korona ambapo alisema yeye tayari amechanja na hajapata madhara yoyote hivyo wananchi wasiwe na hofu bali waende kupata chanjo.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Dkt. Boniface Kasululu akitoa mada kuhusu utekelezaji wa mpango harakishi wa uhamasishaji na utoaji wa chanjo dhidi ya UVIKO -19 juzi kwenye kikao cha kamati ya Afya ya Msingi Mkoa kilichofanyika Sumbawanga.
………………………………………………………………….
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti ameagiza watendaji wa vijiji, kata na tarafa kupatiwa elimu juu ya umuhimu wa kuchanja chanjo dhidi ya ugonjwa wa korona ili hatimaye wahamasishe jamii kujitokeza kupata chanjo hiyo kwenye maeneo yao.
Mkirikiti aliyasema hayo juzi (24.09.2021) akifungua kikao cha kamati ya Afya ya Msingi ya Mkoa kuhusu utekelezaji wa mpamgo harakishi wa uhamasishaji wananchi kujitokeza kupata chanjo dhidi ya UVIKO-19 mjini Sumbawanga.
“Nataka kuona mifumo ya serikali sasa iongee kuanzia Mwenyekiti wa kijiji, mtaa pia viongozi wa kata na tarafa wawezeshwe ili wafanye kazi ya kushawishi wananchi kwenda vituo vya afya kuchanja kwani wana nguvu na wanaaminika na umma” alisema Mkirikiti.
Mkuu huyo wa Mkoa alisema viongozi ngazi zote wana wajibu wa kwenda kuliponya taifa dhidi ya maambukizi ya korona kwa kuamua kuchanja pamoja na kuwahamasisha wananchi kwenye maeneo yao ikiwemo taasisi zote za umma, vyama vya siasa, madhehebu ya dini na sekta binafsi.
Akitoa taarifa ya mkoa kuhusu mwenendo wa utoaji chanjo dhidi ya uviko Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Dkt. Boniface Kasululu alisema tayari dozi 4,000 kati ya 20,000 zilizopokelewa zimetumika kwa watu kuchanja ambapo zoezi linaendelea.
Aliongeza kusema chanjo zilizopokelewa zinatakiwa kuwa zimemalizika ifikapo mwezi wa Novemba hivyo viongozi wana wajibu wa kuhamasisha wananchi kwenda kupata chanjo kwenye vituo vya kutolea huduma.
Ili kufikia lengo la watu wengi kupata chanjo, Dkt. Kasululu alisema mkoa umeandaa mpango wa utoaji mafunzo kwa watoa huduma za afya ngazi ya halmashauri na mkoa ili wakafanye kazi ya kuhamasisha wananchi kupata chanjo ya UVIKO -19.
Kwa upande wake Kiongozi wa Machifu wa Rukwa Charles Katata Milanzi aliyeshiriki kikao hichi kwa niaba ya machifu wenzake alisema wananchi wanahitaji elimu kwa karibu ili wajitokeze kupata chanjo dhidi ya UVIKO 19.
Chifu huyo alisema yeye tayari amechanja na kuwa anajisikia vemana sasa anahamasisha wenzake pamoja na wananchi kujitokeza kupata chanjo ya kujikinga naugonjwa wa korona.
“Sisi tunao mchango mkubwa ,wenzagu waliposikia nimechanja waliingiwa na imani kuwa chanjo hii ni salama na haina madhara yoyote mwilini” alisema Chifu Milanzi.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Amani mkoa wa Rukwa na Askofu wa KKKT Dayosisi ya Ziwa Tanganyika Askofu Ambele Mwaipopo alisema suala la kuhamasisha wananchi kujitokeza kupa chanjo ya UVIKO 19 ni jambo la kufa na kupona na muhimu kipindi hiki ili kuliponya taifa.
“Ni aibu sana chanjo 20,000 tulizoletewa na serikali zisizpoisha. Hii ni changamoto kwetu viongozi tumepewa bure tuhakikishe zinawafikia wananchi wote kwani ni mpango wa Mungu kutunusuru sisi viumbe wake na janga hili la korona “alisisitiza Askofu Mwipopo
Askofu huyo wa KKKT aliongeza kusema chanjo ya dhidi ya UVIKO -19 ni salama kwani toka amechanja hadi leo hajaona madhara yoyote hivyo wananchi wajitokeze na kupata chanjo ili wajiepushe na maambukizi ya ugonjwa wa korona .
Mwisho
Imeandaliwa na:
Afisa Habari Mkuu,
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa
SUMBAWANGA
26.09.2021