*****************************
Na John Walter-Manyara
Afya ya uzazi ni suala ambalo ni muhimu katika jamii yoyote, lakini upatikanaji wa huduma hii hukabiliwa na changamoto mbalimbali na hivyo kuwaweka wasichana na wanawake katika mazingira magumu.
Nchini Tanzania juhudi za serikali zinasaidia kulinda wasichana na wanawake katika kupata huduma muhimu za afya ya uzazi lakini pia mashirika yasiyo ya kiserikali yanaziba pengo ambalo linasalia.
Taarifa kutoka nchi 57 nyingi zikiwa za kusini mwa Jangwa la Sahara barani Afrika zinaonesha kwamba ni nusu tu ya wasichana waliokwisha balekhe na wanawake ndio wana fursa ya kujifanyia maamuzi binafsi,kuhusu miili yao na uhuru kwa ujumla wa kuamua chochote.
Hapa uhuru unaozungumziwa unajumuisha pia masuala kama kutumia njia za mpango wa uzazi.
Hii ni ripoti iliyochapishwa na shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na idadi ya watu UNFPA.
Klabu ya Waandishi wa Habari mkoa wa Manyara (MNRPC) imekuja na mradi wa Afya ya Wanawake na Wasichana unaodhaminiwa na shirika lisilo la kiserikali la Women Fund Tanzania (WFT) kwa ajili ya uelimishaji juu ya haki ya Afya ya uzazi iliyolenga maeneo mawili ya Kata ya Endasak wilayani Hanang na Kata ya Sigino Halmashauri ya mji wa Babati, mradi utakaodumu kwa muda wa miezi sita.
Mratibu wa mradio huo Jaliwasson Jason amesema adhma yao ni kuhakikisha wanaungana waandishi wa habari walipo katika klabu hiyo na kutoa elimu kwa jamii ili ibadilike na kuacha kufanya ukatili ikiwemo kwa Wanawake na Wasichana.
Akitoa elimu kwa baadhi ya Wasichana na Wanawake katika kijiji cha Endasak wilayani Hanang, Afisa ustawi wa Jamii wilayani hapo Martha Sulle amesema visa vya kikatili kwa Wanawake,wasichana na hata watoto vimekuwa vikiripotiwa katika wilaya hiyo.
Amewataka Wanawake pamoja na wasichana kutoa taarifa ofisi za Ustawi wa jamii au Polisi pindi anapofanyiwa kitendo cha ukatili na sio kumaliza Kinyumbani kama wanavyofanya baadhi yao ili hatua zinazostahili zichukuliwe kwa wahusika.
Hata hivyo baadhi ya Wanawake wameeleza kuwa wamekuwa wakipata maudhi katika miili yao baada ya kutumia njia za uzazi wa mpango ikiwa ni pamoja na kukosa hamu ya kushiriki tendo na waume zao,kunenep kupita kiasi au kuvimba miguu.
Mtaalamu wa afya ya Uzazi kutoka hospitali ya Tumaini Hanang Anasia Mariki amekiri kutokea maudhi madogo madogo kwa baadhi ya watumiaji wa njia za uzazi wa mpango huku akiwataka wanapata mabadiliko kufika hospitali ili kushauriwa njia sahihi ya uzazi wa mpango.
Mariki amesema zipo njia za muda mfupi, mrefu na hata za kudumu za uzazi wa mpango.
Amezitaja njia za muda mfupi ni Sindano,vidonge,kondomu huku akibainisha za muda mrefu ni njiti zinazowekwa mkononi ambazo zipo za miaka mitatu,mitano,kitanzi kinachoekwa kwenye mji wa mimba cha hadi miaka kumi.
Amesema njia za kudumu ni pamoja na kufunga kizazi kwa Baba au mama pale wanapojiridhisha kuwa idadi ya watoto watoto waliohitaji imefikia mwisho.
Wanawake na wasichana wengi wananyimwa uhuru wa kujiamualia juu ya kutumia njia za kupanga uzazi, wanapangiwa mwanaume wa kumuoa, wanalazimishwa kupitia ukeketaji wakati wengine wakiozwa katika umri mdogo.
Attachments area