RC
Nchimbi akikabidhi zawadi ya Rozari Takatifu kwa vijana waliohudhuria Kongamano
la Kumbukizi ya Mwalimu Nyerere Singida jana.
Mratibu wa Kongamano hilo na Afisa wa Vijana kutoka Ofisi ya
Mkuu wa Mkoa, Frederick Ndahani akizungumza na vijana wa mkoa huo kabla ya
kumkaribisha RC Nchimbi kufungua Kongamano la Kumbukizi ya Baba wa Taifa,
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere jana.
Vijana
wakishiriki kikamilifu Kongamano hilo.
Na Godwin Myovela, Singida
MKUU wa Mkoa wa Singida Dk. Rehema Nchimbi ametoa zawadi ya
Rozari Takatifu kwa mamia ya vijana mkoani hapa, lengo ni kuwahamasisha vijana
hao kumkimbilia Bikira Maria kwa sala katika kipindi hiki cha mwezi wa Rozari,
lakini pia kwa maombezi yake aweze kulivusha salama Taifa katika uchaguzi mkuu
ujao
Nchimbi alikabidhi rozari hizo muda mfupi baada ya kufungua
Kongamano la Vijana katika Kumbukizi ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, lililofanyika
kwenye ukumbi wa chuo cha uhasibu, mkoani hapa jana.
“Zawadi pekee ninayoweza kuwapa leo hii ni hizi Rozari
Takatifu, huu ni mwezi wa rozari kwa mama yetu na kipenzi chetu Bikira Maria.
Naamini tukimkimbilia kwa lolote atatusaidia, tutavuka salama,” alisema Nchimbi.
Kila ifikapo mwezi Oktoba waamini Wakatoliki hualikwa kusali
Rozari kwa mwezi mzima, lengo likiwa ni kumuheshimu na kumshukuru Bikira Maria
kwa maombezi yake ya kimama kwa wanadamu. Lakini ni fursa pia ya kumwendea na
kumshirikisha furaha, shukrani, taabu, changamoto na matarajio.
Aidha, sala ya Rozari Takatifu hutoa nafasi ya kutafakari
mafumbo ya maisha ya Yesu Kristu na Maria, katika safari ya wokovu wa
mwanadamu.
Kwa wakatoliki na marafiki wa karibu wa Bikira Maria,
akiwemo mama Nchimbi, huamini kuwa Rozari ni sala nzuri sana na yenye utajiri
wa Neema, ni sala inayogusa kwa karibu Moyo safi wa Mama huyo wa Mungu, lakini pia
ni chanzo cha kutamalaki kwa amani katika familia, jamii, taifa na ulimwengu
mzima.