Naibu Waziri wa Kilimo Omary Mgumba ,akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati akitoa taarifa kuhusu Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani Kitaifa yatafanyika Mkoani Njombe.
Naibu Waziri wa Kilimo Omary Mgumba akitoa taarifa rasmi ya serikali kuhusu kufanyika kwa Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani yatakayofanyika kitaifa mkoani Njombe kuanzia 10 Oktoba mwaka huu.Kulia ni Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya.
…………………………………………………………………………………………………….
Na.Alex Sonna,Dodoma
Serikali imesema maadhimisho ya siku ya chakula duniani yatafayika kitaifa mkoani Njombe ambapo yanalenga kuhamasisha jamii kuwa na uhakika wa chakula na lishe bora.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Kilimo Omary Mgumba alipokuwa akitoa taarifa kwa waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya siku ya Chakula Duniani ambapo kitaifa yatafanyika mkoani Njombe kuanzia Oktoba 10 hadi 16.
“Kwa wakazi wa mkoa wa Njombe na mikoa jirani ya Nyanda za Juu Kusini nawaomba mjitokeze kwa wingi kwenye maadhimishoambayo yatazinduliwa rasmi kitaifa tarehe 10/10/2020 na kufikia kilele chake tarehe 16 Oktoba, 2020 mkoani Njombe” amesema Mgumba
Mgumba amesema kuwa kila mwaka Makao Makuu ya Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) huzitaka nchi wananchama kuhamasisha wadau wote wa Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kuchangia katika kuhakikisha kila mtu anawezeshwa kupata chakula bora na cha kutosha wakati wote wa maisha yake.
Alibainisha kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu inasema ” Kesho Njema Inajengwa na Lishe Bora Endelevu” ambapo ameipongeza seriklai ya awamu ya Tano kwa kuitekeleza kwa vitendo kauli mbiu hiyo upande wa uzalishaji mazao ya chakula.
”Tathmini iliyofanyika hivi karibuni ya uzalishaji kwa msimu wa 2019/2020, inaonesha kuwa uzalishaji wa mazao ya chakula unatarajia kufikia tani 17,742,388 ambapo mahitaji ni tani 14,347,955. Mahitaji haya yakilinganishwa na uzalishaji nchi inategemewa kuwa na ziada ya tani 3,511,620 za chakula ambapo tani 1,322,020 ni za mazao ya nafaka na tani 2,072,413 ni za mazao yasiyo nafaka” amesisitiza Mgumba.
Kuhusu tatizo la lishe bora linalopelekea udumavu, Mgumba amesema kuwa takwimu zinaonesha kuwa udumavu umepungua kutoka asilimia 42 mwaka 2010 hadi asilimia 32 mwaka 2018 na ukondefu umepungua kutoka asilimia 3.8 mwaka 2014 hadi asilimia 3.5 mwaka 2018 ambayo ni chini ya kiwango cha malengo ya Mkutano wa Afya Duniani (WHA) cha asilimia 5.
Mgumba alitaja mikoa inayozalisha chakula kwa wingi ndiyo yenye viwango vikubwa vya udumavu kwa watoto kwa mfano Njombe ina udumavu wa asilimia 53.6 wakati uzalishaji mazao ni tani 446,491 kuwa na kiwango cha utoshelevu- SSR asilimia 194 na mkoa wa Rukwa asilimia 47.9, huku uzalishaji ni tani 943,002 na kiwango cha Utoshelevu-SSR asilimia 230.
Iringa ina udumavu wa asilimia 47.1, huku uzalishaji ni tani 470,750 na kiwango cha utoshelevu-SSR asilimia 161 na Songwe ina udumavu asilimia 43.3 huku uzalishaji mazao ni tani 805,545 na kiwango cha utoshelevu cha asilimia 210.
Aidha Mumba amesema kuwa hali hii ya udumavu ndio imepelekea Wizara ya Kilimo na wadau kkutana mkoani Njombe pamoja na kuhamasisha uzalishaji mazao ya chakula elimu ya lishe bora kutoka kwa wataalam itatolewa katika siku zote saba ikiwemo uhamasishaji ulaji vyakula vya asili yenye protini nyingi.
Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya amesema kuwa kamati ya maadalizi ya maadhimisho hayo ngazi ya taifa na ile ya mkoa wa Njombe zimefanya kazi nzuri kuhamasisha wadau zikiwemo taasisi za umma na binafsi kujitokeza kushiriki
Kusaya amesema kuwa wizara ya kilimo inaendelea kutoa wito kwa wadau zaidi kujitokeza kwenye maadhimisho ya mwaka huu na kuwa yanalenga kuwawezesha wakulima na wananchi kujua kanuni bora za uzalishaji mazao ya chakula,uhifadhi,teknolojia ya uongezaji thamani na elimu ya masuala ya lishe bora.
‘ Tunawashukuru wadau wetu FAO,WFP,UNICEF.Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Njombe,BRITEN,Licolto,Wizara ya Mifugo na Uvuvi,Wizara ya Afya kwa ushrikiano wao kwa wizara ya Kilimo kuandaa maadhimisho ya mwaka huu” amesema Kusaya.
Maadhimisho ya mwaka huu ni ya 40 tangu yalipoanza kuadhimishwa mwaka 1945 na Shirika la Chakula na Kilimo la Umaoja wa Mataifa (FAO) .Maadhimisho ya siku ya chakula mwaka uliopita yalifanyika mkoani Singida