*******************************
Na Ahmed Mahmoud Arusha
Mkuu wilaya ya Arusha Kenan Kihongosi ameunda tume ya kufuatilia mgogoaro wa ubadhirifu fedha kwenye vya bodaboda ndani ya jiji la Arusha ambavyo ni Uwapa na Uboja.
Kihongosi ameunda tume hiyo mara baada ya kukutana na waendesha bodaboda ndani ya jiji la Arusha na kubaini uwepo wa ufujaji wa fedha mara baada ya kupokea malalamiko hayo kutoka kwa waandesha bodaboda hao waliowasilosha kwake katika uwanja wa shekhe Amri Abeid jijini Arusha.
Aidha aliwataka waendesha bodaboda hao kuwa wazalendo kwa nchi yao na kuhakikisha wanalinda amani ya taifa lao ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa za uvunjifu wa amani katika maeneo yao.
Alisema kuwa serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt.John Magufuli haitakubali kuona viongozi wachache wakifuja fedha za wananchi nao kuwaachi hivi hivyo kuitaka tume hiyo kufuatilia kwa kina na kuja na majawabu yatakayomaliza mgogoro huo
Alibainisha kuwa yeye hayupo kisiasa bali yupo kushughulikia shida za wananchi ndio maana amekutana nao ili kumaliza tofauti zao kwa lengo la kuwasaidia kuongeza tija katika majukumu yao na kuwaondolea kero zinazowakabili hilo ndio jukumu langu kubwa.
Alisema kuwa serikali itasimamia kuona makosa ambayo yanastahili kupewa onyo kwani imetambua uwepo wa uvunjifu wa sheria hivyo kuwataka madereva bodaboda kuendelea kufuata sheria na serikali itawasaidia kwenye makosa madogo kupewa onyo badala ya kutozwa faini kubwa na wapo kuondoa changamoto zao ndogondogo.
“Niwasihi sana kuendeleza utulivu na amani kwani serikali yenu ipo pamoja nanyi kuhangaika na shida zenu na tutahakikisha kumaliza mgogoro huu ili kuwasaidia kuunda umoja imara wenye maslahi kwenu”
Kwa upande wake Mwenyekiti wa tume hiyo wakili Albert Msando ameahidi kuanza mara moja kupokea maoni na changamoto ili kuzipatia ufumbuzi wa haraka na kuwasilisha mapendekezo kwa mkuu wa wilaya ndani ya muda mfupi.
Alisema kuwa anatambua changamoto kubwa atakayoanza nayo ni katiba ya umoja huo kwani kumekuwa hakuna uongozi unaojali maslahi mapana ya waendesha bodaboda hao hivyo kuwepo mianya ya ubadhirifu.
Alisema kuwa kwa msingi huo katiba itakuwa ndio suluhu ya kudumu ambayo itasaidia kuwepo uwazi kwenye matumizi ya fedha ndani yao na itasaidia kujua ukomo wa uongozi na mipaka yao na hivyo itasaidia kuondoa migogoro ambayo siyo ya lazima.