Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akikagua eneo linalojengwa bweni la wasichana katika shule ya sekondari ya Misungwi.
Moja ya jengo la bweni la wasichana katika shule ya sekondari Misungwi lililojengwa na serikali kupitia mradi wa EP4R.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako akimkabidhi ngao ya pongezi Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Misungwi, Mwanani Asembandwa baada ya kuwa shule ya kwanza mkoa wa Mwanza katika matokeo ya kidato cha sita 2019.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akizungumza na wanafumzu wa Shule ya Sekondari Misungwi alipofika shuleni hapo kukagua mindombinu ya shule hiyo.
Muonekano wa moja ya jengo la madarasa ya shule ya sekondari Misungwi iliyojengwa na serikali kupitia Mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R)
……………….
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako ameahidi kutoa shilingi milioni 31 kwa shule ya Sekondari Misungwi ili kukamilisha ujenzi wa bweni linalojengwa na shule hiyo.
Waziri Ndalichako ametoa ahadi hiyo mwishoni mwa wiki alipofika shuleni hapo kukagua miundombinu ya shule hiyo ambapo Serikali imejenga madarasa mapya, maabara na Bweni yaliyowezesha wanafunzi kuongeza ari ya kusoma na kupelekea shule hiyo Kuongoza katika mtihani wa kidato cha sita Mkoani Mwanza na kuongeza idadi ya wanafunzi.
Ndalichako akiwa shuleni hapo amesema amefurahishwa kuona uongozi wa shule hiyo umekuwa ukitumia fedha vizuri na kuweka akiba kidogokidogo kwa miaka mitatu ambapo kupitia kupitia akiba hiyo wamepata fedha ambazo zimewawezesha kuanza ujenzi wa bweni jipya.
“Nimefurahishwa na mpango wa shule wa kuhifadhi fedha kidogo kidogo mpaka wamepata fedha kwa ajili ya ujenzi wa bweni la watoto wa kike jitihada hizi ni lazima ziungwe mkono nami nikiwa waziri mwenye dhamana ya elimu natoa ahadi ya kuleta fedha za kumalizia huu ujenzi ” Alisema waziri Ndalichako.
Profesa Ndalichako amesema pamoja na kutoa fedha kwa ajili ya kumalizia ujenzi pia atahakikisha samani za bweni hilo jipya zinanuliwa ili likamilike na kutumika kwa wakati.
Aidha, Waziri Ndalichako amewata wanafunzi katika shule hiyo kuzingatia masomo na kutojiingiza katika mambo ambayo yatawakatisha masomo na mwisho kutofikia ndoto zao.
Mkuu wa Shule ya sekondari Misungwi Mwanani Asembandwa amemshukuru Waziri wa Elimu kwa kutambua jitihada za shule za kuweka fedha kidogokidogo kwa ajili ya ujenzi wa bweni la wasichana
Asembandwa amesema shule hiyo imefanikiwa kuwekeza fedha kidogo kidogo mpaka ikafanikiwa kupata shilingi miliini 44 ambazo zimetumiwa kuanza ujenzi wa bweni la wasichana ambalo likikamilika litakuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 80 kwa wakati mmoja.
“Kukamilika kwa bweni hili kutasaidia kutatua changamoto ya sehemu ya kulala kwa wanafunzi wetu kufuatia ongezeko pamoja na kuongeza wigo wa kutoa elimu katika mazingira bora”amesema Mkuu huyo wa Shule.
Naye Mwanafunzi wa shule hiyo Zemda Robert amemshukuru Waziri kwa kutoa ahadi hiyo ambayo inakwenda kupunguza changamoto ya malazi shukeni hapo ambapo wameahidi kuongeza bidii ya kusoma na hivyo kuongeza ufaulu.